IQNA

Miili ya Waislamu waliouawa katika vita vya Bosnia yapatikana katika kaburi la umati

9:19 - June 09, 2019
Habari ID: 3471991
TEHRAN (IQNA)- Mabaki ya miili ya Waislamu 12 ambao waliuawa katika vita vya ndani vya Bosnia kati ya mwaka 1992-95 yamepatikana katika kaburi la umati karibi na mji wa Sarajevo.

Takribani watu 100,000, wengi wao wakiwa ni Waislamu, waliuawa katika vita vya Bosnia na hadi sasa wengi 7,000 hawajulikani waliko.

Kwa mujibu wa Emza Fazlic, msemaji wa Taasisi ya Bosni ya Watu Waliotoewa, ushahidi unaonyesha kuwa Waislamu hao waliuawa wakati wakijaribu kukimbilia maeneo salama.

Miili hiyo sasa imepelekwa katika eneo maalumu karibu na mji wa Sarajevo kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa vinasaba au DN ili kubainia familia zao. Wakati vita vya Bosnia vilipomalizika, watu 31,500 walikuwa hawajulikani waliko na tokea wakati huo hadi sasa miili 25,000 imefukuliwa kutoka makaburi ya umati. Katika tukio moja pekee, zaidi ya wanaume na wavulana 8,000 Waislamu waliuawa kikatili katika oparesheni ya askari wa Kiserbia  katika mauaji ya Srebrenica Julai 1995. Mauaji hayo yalitajwa kuwa mabaya zaidi barani  Ulaya tokea Vita Vikuu vya Pili vya Dunia na yalitambuliwa kuwa ni mauaji ya kimbari.

Machi mwaka 2016 Mahakama ya Kimataifa ya Yugoslavia ya Zamani ICTY ilimhukumu kifungo cha miaka 40 jela Radovan Karadzic aliyekuwa kiongozi wa zamani wa Serbia ambaye alipatikana na hatia ya kuua Waislamu 7,000.

Mahakama hiyo yenye makao yake The Hague ilimpata Karadzic na hatia ya mauaji ya kimbari ya Srebrenica.

Mwaka 2017 ICTY ilimhukumu kifungo cha maisha jela Jenerali Ratko Mladic, aliyekuwa kamanda wa kijeshi wa Serbia baada ya kupatikana na hatia ya kuagiza kuuawa maelfu ya Waislamu huko Srebrenica mwaka 1995.

Umuhimu wa suala la mauaji ya Srebrenica unatokana na kuwa, mauaji hayo yalitokea mbele ya macho ya vikosi vya Uholanzi vilivyokuwa sehemu ya kikosi cha kusimamia amani cha Umoja wa Mataifa  na yalitokea katika eneo ambalo lilitangazwa na Umoja wa Mataifa kuwa ni eneo salama na vilevile Umoja wa Mataifa ulikuwa umechukua jukumu la kulinda eneo la Srebrenica kwa mujibu wa maazimio yaliyokuwa yamepasishwa na Baraza la Usalama.

3468694

captcha