Katika ujumbe wa salamu za Idi aliowatumia viongozi wa nchi za Kiislamu hii leo, Rais Hassan Rouhani amesema, ana matumaini kwamba, kwa kushikamana na nuru ya uongofu ya Qur’ani na kwa kufuata Suna za Mtume wa rehma (SAW), Ulimwengu wa Kiislamu utaweza, kwa kushirikiana pamoja, kudhibiti umwagaji damu na mielekeo ya kufurutu mpaka katika zama ambazo wanadamu wanahitajia zaidi utulivu na amani kuliko wakati mwengine wowote ule. Naye Spika wa Bunge Ali Larijani, sambamba na kuwapa mkono wa Idi Maspika wa Mabunge ya nchi za Kiislamu amesisitiza kwamba somo kubwa la Hija na amali za ibada hiyo tukufu ni kuimarisha moyo wa udugu, umoja na kuwa kitu kimoja chini ya bendera ya tauhidi. Waislamu ulimwenguni kote kesho watasherehekea Sikukuu ya Idul-Adh’ha.