Kwa mujibu wa mwandishi wa Shirika la Kimatiafa la Habari za Qur'ani (IQNA), nyaraka hizo zinaonyesha kuwa mahujaji wapatao 7,477 walipoteza maisha katika maafa ya Mina. Aidha nyaraka hizo zinaonyesha kuwa watu 1,508 hawajaweza kubanika utambulisho wao.
Katika hali ambayo Saudi Arabia hadi sasa haijatangaza rasmi idadi ya raia wake waliopoteza maisha katika maafa ya Mina, nyaraka hizo za Wizara ya Afya ya Saudia zinaonyesha kuwa Wasaudi 1,528 walipoteza maisha katika maafa hayo.
Maafa ya eneo la Mina yalijiri tarehe 24 Septemba katika siku kuu ya Idul Adha wakati mahujaji walipokuwa katika amali ya kupiga mawe shetani ijulikanayo kama Ramy al-Jamarat karibu na mji mtakatifu wa Makka. Tokea wakati wa tukio hilo Saudi Arabia imekuwa ikisisitiza kuwa ni watu 769 walipoteza maisha. Takwimu hizo hazikujumuisha mahujaji ambao hadi sasa hawajulikani waliko.
Nyaraka hizo zimebainisha majina kamili, umri na utaifa wa waliopoteza maisha.
Mwezi moja baada ya maafa ya kusikitisha ya Mina, utawala wa Saudi Arabia haijaonyesha uwazi kuhusu kupoteza maisha na kujeruhiwa maelfu ya Waislamu katika ibada ya Hija. Ili kutizama nyaraka hizo za siri za Wizara ya Afya Saudi Arabia, bonyeza hapa.../mh