Katika maandamano hayo yaliyofanyika leo Jumapili katika Medani ya Al Sabin mjini Sana'a, Wayemen walikuwa wamebeba bendera za nchi yao huku wakitoa nara dhidi ya umwagaji damu wa Saudia nchini humo kwa muda wa miaka miwili.
Akizungumza katika maandamano hayo, Saleh al Samad, Rais wa Baraza Kuu la Kisiasa la Yemen amewapongeza Wayemen kwa kusimama kidete na kupmabana na wavamizi Wasaudi. Amesema Saudi imeshindwa kufikia malengo yake nchini Yemen pamoja na kuwa imetumia kiasi kikubwa cha fedha na silaha za kisasa.
Lengo kuu la hujuma ya Saudia dhidi ya Yemen ni kumrejesha madarakani kibaraka wake, Rais mtoro na aliyejiuzulu wa nchi hiyo Abd Rabu Mansour Hadi na kuwaondoa madarakani wanamapinduzi wa Ansarullah.
Tangu ulipoanzisha uvamizi wake wa kijeshi dhidi ya Yemen mwezi Machi mwaka 2015, hadi sasa muungano vamizi wa kijeshi unaoongozwa na utawala wa Aal Saud na kuungwa mkono na Marekani na Israel zaidi ya watu 12,000 wamepoteza maisha katika hujuma ya kinyama ya Saudia dhidi ya Yemen. Kwa mujibu wa televisheni ya Al Masira kati ya waliopoteza maisha katika hujuma ya Saudia ni watoto 2, 646 na wanawake 1,922.
Aidha umeshazishambulia skuli, hospitali, makaazi ya raia, barabara, masoko na kambi za wakimbizi na kuua maelfu ya raia wasio na hatia wa nchi hiyo. Ndege za kivita za Saudia aidha zimebomoa nyumba za raia zipatazo 403,039 na misikiti 712.
Wakati huo huo, Harakati ya Ansarullah ya Yemen imesema utawala wa kifalme wa Aal-Saud umeshindwa kupata natija katika mashambulizi yake ya kinyama dhidi ya nchi hiyo ya Kiarabu na jirani yake.
Hayo yamesemwa na kiongozi wa Ansarullah, Abdul-Malik Badreddin al-Houthi katika hotuba ya jana, kwa mnasaba wa miaka miwili tangu Saudi Arabia iivamie Yemen na kuanzisha mashambulizi ya anga ya kila siku.
Al-Houthi amesisitiza kuwa, licha ya Riyadh na waitifaki wake kutumia silaha za maangamizi dhidi ya raia wa Yemen, lakini wananchi hao wamesimama kidete na kusimama pamoja dhidi ya utawala huo wa kifalme.