IQNA

Wapalestina waswali Sala ya Idul Adha katika Msikiti wa Al Aqsa

10:23 - August 22, 2018
Habari ID: 3471642
TEHRAN (IQNA)- Maelfu ya Wapalestina Jumanne wameswali Sala ya Idul Adha katika Msikiti wa Al Aqsa ulio katika mji wa Quds (Jerusalem) unaokaliwa kwa mabavu na utawala wa Kizayuni wa Israel.

Katika hotuba yake ya Sala ya Idul Adha, Imamu wa Msikiti wa Al Aqsa Sheikh Muhammad Hussein amesisistiza kuwa Wapalestina wana azma imara ya kulinda Quds Tukufu na Msikiti wa Al Aqsa mbele za njama za Uyahudishaji za utawala haramu wa Israel.

Kwa mujibu wa Faras Debs, afisa katika Idara ya Wakfu ya Quds Tukufu, takribani waumini 100,000 walifanikiwa kuswali Sala ya Idul Adha katika Msikiti wa Al Aqsa pamoja na kuwepo vizingiti vingi vilivyowekwa na wanajeshi wa utawala wa Kizayuni ambao waliwazuia vijana Wapalestina kuswali.

Leo tarehe 10 Mfunguo Tatu Dhul-Hija ni sikukuu ya Idul Adh'ha, moja ya sikukuu kubwa za Kiislamu. Katika siku hii mahujaji wa Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu waliokwenda Makka, huchinja mnyama kwa ajili ya kutekeleza amri ya Mola wao na kuhuisha kumbukumbu ya Nabii Mtukufu Ibrahim AS.

Mwenyezi Mungu aliijaribu imani na ikhlasi ya Nabii Ibrahim AS na kumwamuru amchinje mwanawe kipenzi Ismail (as). Licha ya mashaka ya utekelezwaji wa amri hiyo, Nabii Ibrahimu (as) aliandaa mazingira ya kutekeleza amri hiyo na kumlaza chini mwanaye na kuanza kuikata shingo yake lakini kisu kilikataa kuchinja. Hapo ndipo alipoambiwa na Mwenyezi Mungu kuwa amefaulu mtihani huo na akamtumia mnyama wa kuchinja badala ya mwanaye Ismail.

374045

captcha