IQNA

Inna Lillah wa Inna Ilayhi Rajioun

Mtoto wa miaka 6 achinjwa Madina, Saudia katika tukio la chuki za kimadhehebu

20:39 - February 09, 2019
Habari ID: 3471835
TEHRAN (IQNA)-Mtu mwenye chuki za kimadhehebu amemuua mtoto aliyekuwa na umri wa miaka sita, mbele ya mama yake katika mji mtakatifu wa Madina nchini Saudi Arabia.

Taarifa zinasema mtoto huyo aliuawa kikatili na derava wa teksi mjini Madina mwishoni mwa mwezi uliopita wa Januari, katika kile kinachoonekana ni mauaji ya chuki za kimadhehebu.
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo amenukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa, dereva huyo wa teksi alipandwa na hasira kufuatia na kitendo cha mama ya mtoto huyo kwa jina Zakariya Bader al-Jabir, ambaye ni wa madhehebu ya Shia, kumsalia Mtume (SAW) na Aali zake, na hapo ndipo alimvuta kwa nyuma na kumchinja mbele ya mama yake.
Taarifa zinasema mama na mtoto wake huyo mvulana walichukua teksi kuelekea katika mji mtukufu wa Madina kwa ajili ya kufanya ziara, na baada ya dereva wa teksi kugundua kuwa ni Mashia, alisimamisha gari ghafla mkabala wa mgahawa mmoja ulioko karibu na eneo la al-Tilal.
Baada ya kupiga breki dereva huyo alimshusha kwa nguvu kijana huyo kutoka kwenye gari, na kisha akavunja chupa ya glasi na kumkaka shingo lake mbele ya mama yake.
Polisi nchini Saudi Arabia wanadai dereve aliyetekeleza ukatili huo alikuwa na matatizo ya kisaikolojia ili kujaribu kufunika jinai hiyo na kumpunguzia adhabu.
Mauaji ya mtoto huyo mdogo ni natija ya itikadi potovu za Uwahhabi zinazotawala Saudia Arabia. Mawahhabi wanaamini kuwa Waislamu wa madhehebu ya Shia na hata Waislamu wa madhehebu ya Sunni wasiofuata itikadi zao ni makafiri na ni halali kuwaua. Fikra hii ya Uwahhabi inafuatwa na aghalabu ya makundi ya magaidi wakufurishaji duniani kama vile ISIS au Daesh, Al Qaeda, Al Shabab, Boko Haram n.k.

3467889

captcha