IQNA

Ujumbe wa Kiongozi Muadhamu kwa Mnasaba wa Mwaka wa 40 wa Ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu

12:58 - February 14, 2019
Habari ID: 3471841
TEHRAN (IQNA) Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Jumatano ametoa ujumbe muhimu sana kwa taifa la Iran kwa jina la "Hatua ya Pili ya Mapinduzi" kwa mnasaba wa maadhimisho ya miaka 40 ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ametoa ujumbe huo Jumatano na kusisitiza kuwa Mapinduzi ya Kiislamu na taifa la Iran lina nguvu na ni imara lakini wakati huo huo lina huruma na uvumilivu bali hata ni madhlumu. Ameongeza kuwa, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran hayajawahi kuwa ya kwanza kufyatua risasi hata katika kupambana na Marekani na Saddam, bali katika matukio yote, taifa la Iran na Mapinduzi ya Kiislamu yamesimama imara kujihami na kutoa majibu makali kila pale adui anapoanzisha mashambulizi.

Kiongozi Muadhamu, katika sehemu ya ujumbe wake alisema: "Mapinduzi ya kihamasa ya taifa la Iran, ni Mapinduzi makubwa zaidi na yaliyoungwa mkono zaidi na wananchi katika zama hivi. Ni Mapinduzi pekee ambayo katika muongo wake wa 40,  yemaweza kudumisha fahari pasina kusaliti malengo yake na yameweza kulinda heshima yake na nara zake za asili pamoja na kuwepo kila aina ya vishawishi ambavyo vilionekana kuwa haviwezi kuepukika. Mapinduzi hayo sasa yanaingia katika hatua yake ya pili ya ustawi, kujijenga kijamii na kujenga ustaarabu mpya.

Vile vile katika ujumbe wake huo ametaja mafanikio mbalimbali ya Mapinduzi ya Kiislamu akisema kuwa mafanikio muhimu zaidi ni pamoja na kuimarisha utulivu na usalama nchini Iran, kulinda ardhi na mipaka yote ya nchi, kuanzishwa miundombinu muhimu mno ya kiuchumi na kimaendeleo, kuongezeka kwa wingi ushiriki wa wananchi katika masuala ya kisiasa kama vile chaguzi, kuongezeka mwamko wa kisaisa wa matabaka mbalimbali ya wananchi na mtazamo wao kuhusu masuala ya kimataifa, kugawanywa kiuadilifu suhula za umma nchini, kuongezeka nembo za kimaanawi na kimaadili katika maeneo ya uma kwenye jamii na kusimama imara mbele ya njama za mabeberu na waistikbari wa dunia wakiongozwa na Marekani.

Kiongozi Muadhamu alitaja nukta saba za mambo ya kimsingi ambayo ni lazima yaimarishwe katika hatua hii ya pili ya mapinduzi; kwanza sayansi na utafiti, pili ni  umaanawi na maadili bora, tatu ni uchumi, nne ni uadilifu na kupambana na ufisadi, tano ni uhuru na kujitegemea, sita ni heshima ya kitaifa, uhusiano wa kigeni na kuainisha mipaka kuhusiana na adui na saba ni mtindo wa maisha.

Kuhusu vijana na mustakabali wa Iran ya Kiislamu, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu akasema: "Vijana, kama kizazi kipya cha Mapinduzi, katika kuchukua hatua imara za mustakabali, wanapaswa kufahamu vyema yaliyopita na wapate ibra na darsa kutokana na uzoefu uliopita.

Kiongozi Muadhamu aliashiria nukta ya Iran yenye nuguvu na kusema, leo sawa na zamana za mwanzo wa Mapinduzi ya Kiislamu, Iran ilikabiliana na changamoto za madola ya kibeberu hasa Marekani na Wazayuni lakini sasa mambo yamebadilika na kuna tafauti. Kiongozi Muadhamu amekumbusha kuwa: "Leo changamoto ni katika uwepo wenye nguvu wa Iran katika mipaka ya utawala wa Kizayuni na kusambaratishwa ushawishi haramu wa Marekani katika eneo la Asia Magharibi, na uungaji mkono wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa mapambano ya mujahidina wa Palestina katika kitovu cha ardhi zinazokaliwa kwa mabavu,  na kuhami harakati za Hizbullah na muqawama kote katika eneo. Iwapo zama hizo tatizo la nchi za Magharibi lilikuwa kuizuia Iran kununua silaha za kimsingi, leo wanakabiliana na tatizo la kuzuia silaha zilizostawi na zilizotengenezwa Iran kufikia vikosi vya muqawama. Iwapo katika zama hizo Marekani ilidhani kuwa, kwa kuwategemea Wairani kadhaa wasaliti au helikopta chache, ingeweza kuuangusha mfumo wa Kiislamu na taifa la Iran, leo katika kukabiliana kisiasa na kiusalama na Jamhuri ya Kiislamu, inahitaji muungano mkubwa wa makumi ya serikali hasimu au zilizotiwa hofu lakini pamoja na hayo inafeli katika makabiliano."

3789882

captcha