IQNA

Watoto 80,000 wamekufa njaa Yemen tokea Saudia ianzishe hujuma

14:19 - February 27, 2019
Habari ID: 3471855
TEHRAN (IQNA)-Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema makumi ya maelefu ya watoto Wayemen wamekufa njaa tokea Saudia na waitifaki wake waanzishe vita angamizi dhidi ya nchi hiyo masikini ya Kiarabu.

Akizungumza Jumanne mjini Geneva, Gutteres amesema: "Watoto hawakuanzisha vita dhidi ya Yemen lakini ni waathirika wakuu. Watoto 360,000 wanakabiliwa na hali mbaya ya utapiamlo." Ameongeza kuwa ripoti ya kuaminika inaonyesha kuwa watoto 80,000 walio chini ya miaka 5 wamepoteza maisha Yemen tokea Saudia ianzishe hujuma dhidi ya nchi hiyo mwaka 2015.

Aidha amesema vita vya Yemen vimepelekea wakimbizi wa ndani ya nchi hiyo kuongezeka hadi milioni 3.3 mwaka huu. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametahadahrisha kuhusu hali mbaya ya kibinadamu nchini Yemen na kusema watu milioni 20 nchini humo hawana huduma zinazofaa za afya.

Hivi karibuni pia Baraza la Wakimbizi Norway lilitangaza kuwa Wayemen zaidi ya milioni 20 wanakabiliwa na njaa huku utawala wa Saudi Arabia ukiendelea kuongoza vita dhidi ya nchi hiyo ya Kiarabu ambayo inakabiliwa na maafa makubwa zaidi ya kibinadamu dunaini.

Ripoti hiyo imesema zaidi ya Wayemen milioni 20 kote katika nchi hiyo wanakabiliwa na njaa ambapo nusu yao wanakabliwa na hali mbaya sana ya ukosefu wa chakula. Ripoti hiyo imesema kati ya watu wote milioni 29 wa Yemen, milioni 24 wanahitaji aina fulani ya msaada wa kibinadamu ambapo milioni 14.3 wana mahitajio makubwa. Taarifa hiyo imesema kwa ujumla hali inaendelea kuwa mbaya kote Yemen. 

Inafaa kuashiria kuwa, Saudia ilianzisha mashambulizi dhidi ya Yemen mwishoni mwa mwezi Machi 2015 kwa lengo la kumrejesha madarakani Abdrabbuh Mansour Hadi, rais wa zamani wa nchi hiyo aliyejiuzulu na kutoroka nchi. Hata hivyo Saudi Arabia na washirika wake wameshindwa kufikia malengo yao hayo huku wakisababisha maafa makubwa ya kibinadamu ikiwa ni pamoja na kuwaua raia wasio na hatia. Idadi kubwa ya watoto na wanawake ni miongoni mwa waliopoteza maisha moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja kutokana na vita dhidi ya Yemen vinavyoongozwa na Saudia kwa himaya ya madola ya Magharibi hasa Marekani na utawala haramu wa Israel.

3468016

captcha