IQNA

Iran na Pakistan lazima zistawishe uhusiano hata kama maadui watachukizwa

9:01 - April 23, 2019
Habari ID: 3471924
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, uhusiano wa mataifa mawili ya Iran na Pakistan ni wa moyoni uliokita mizizi vyema na kusisitiza kuwa, uhusiano huo unapaswa kuimarishwa kadiri inavyowezekana hata kama maadui wa mataifa haya mawili watachukizwa na hilo

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei amesema hayo Jumatatu jioni mjini Tehran jioni alipoonana na Imran Khan, Waziri Mkuu wa Pakistan na kuongeza kuwa, masuala ya usalama wa mipakani wa nchi hizo mbili ni muhimu sana.

Kiongozi Muadhamu amebaini kuwa, magenge ya kigaidi yanayovuruga usalama katika mipaka ya nchi hizi mbili yanadhaminiwa kifedha na kisiasa  na maadui na kwamba moja ya malengo yao ya kuchafua usalama katika mipaka ya Iran na Pakistan ni kutaka kuzigombanisha nchi hizi mbili. 

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amegusia uhusiano mkongwe na wa kihistoria wa mataifa mawili ya Iran na Pakistan na kuongeza kuwa, ustawi mkubwa na heshima ya Bara Hindi ilikuwepo katika zama ambazo Waislamu walikuwa wakitawala eneo hilo na pigo kubwa lililotolewa na wakoloni wa Kiingereza dhidi ya watu wa eneo hilo ni kitendo chake cha kuangamiza ustaarabu mtukufu wa Kiislamu wa Bara Hindi.

Aidha ameishukuru serikali ya Pakistan kwa misaada yake kwa wahanga wa mafuriko ya hivi karibuni ya nchini Iran. Kiongozi Muadhamu ameongeza kuwa, hatua ya Waziri Mkuu Imran Khan ya kuanzia safari yake ya kuitembelea Iran ambako alikwenda kufanya ziara katika Haram toharifu ya Imam Ali bin Musa al Ridha AS katika mji wa Mashhad ni ishara nzuri. Amesema Iran ina matumaini kwamba, kwa baraka za Imam Ridha AS safari ya Waziri Mkuu huyo wa Pakistan hapa Iran itakuwa na faida kubwa kwa nchi zote mbili.Iran na Pakistan lazima zistawishe uhusiano hata kama maadui watachukizwa

Kwa upande wake, Waziri Mkuu wa Pakistan amesema katika mazungumzo hayo kwamba kuna watu hawataki kuona uhusiano wa Tehran na Islamabad unastawi.

Waziri Mkuu wa Pakistan ameashiria uhusiano wa kihistoria wa Iran na Bara Hindi na kusema: "Waislamu walitawala India kwa muda wa miaka 600 na taathira ya wairani katika eneo hilo ilikuwa kubwa kiasi kwamba lugha ya Kifarsi ilikuwa lugha rasmi ya serikali ya India."

Halikadhalika amesema, wizi na uporaji mkubwa zaidi ya mali za Bara Hindi ulifanywa katika enzi za ukoloni wa Uingereza na kuongeza kuwa, Waingereza wamepora utajiri wote wa India, wameangamiza mfumo wake wa masomo na walikuwa wanaitaja India kuwa ni koloni lao la vito vya thamani.

Waziri Mkuu wa Pakistan pia ameashiria namna ambayo baadhi hawataki kuona uhusiano wa karibu baina ya Iran na Pakistan lakini akasema pande mbili zinaweza kuvuka tatizo hilo. Ameongoeza kuwa: "Tutajitahidi kuimarisha uhusiano wa nchi mbili na tutaendelea kuwa na mawasliano ya mara kwa mara na serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

3805676

captcha