IQNA

Rais Hassan Rouhani

Iran itaendelea kuuza mafuta kimataifa pamoja na kuwepo mashinikizo ya Marekani

23:22 - April 30, 2019
Habari ID: 3471936
TEHRAN (IQNA) - Rais Hassan Rouhani wa Iran Jamhuri ya Kiislamu amesema nchi hii katu haitasitisha uuzaji wa mafuta ghafi yake ya petroli katika soko la kimataifa pamoja na kuwepo mashinikizo na vikwazo vipya vya Marekani.

Rais Rouhani amesema hayo hii leo hapa Tehran, katika mjumuiko wa kuadhimisha Wiki ya Wafanyakazi Iran na kuongeza kuwa,  njama za  Marekani za kutaka kukata kimilifu uuzaji wa mafuta ghafi ya petrol ya Iran kamwe haitatekelezeka na kwamba katika miezi ijayo, Marekani haitakuwa na jingine ghairi ya kuwa mtazamaji wakati Iran itakapoendelea kuyauza mafuta yake katika soko la kimataifa.

Rais wa Iran amebaini kuwa, "Washington imechukua uamuzi ghalati wa kujaribu kufanya uuzaji wamafuta ya Iran ufikie kiwango cha sifuri, hatutaruhusu hilo lifanyike. Tuna njia zetu nyingi za kuendelea kuuza mafuta nje ya nchi ambazo Marekani haizitambui."

Rais Rouhani ameongeza kuwa, "Lengo kuu la Marekani la kuiwekea Iran vikwazo vya kikatili ni kutaka kufuta mapato ya nje ya taifa hili, lakini kwa uwezo wa Allah, tutaipigisha magoti Marekani."

Amesisitiza kuwa, kusimama kidete dhidi ya Washington ndio wajibu na jukumu kuu la serikali na taifa la Iran.

Rais Rouhani amebaini kuwa, "baadhi ya nchi za zimelegeza msimamo mbele ya mashinikizo ya Marekani na nukta hii imepelekea Marekani iongeze mashinikizo yake. Lakini taifa la Iran liliweza kusimama kidete mbele ya Marekani na kufanikisha mapinduzi yake. Leo pia tutasimama kidete mbele ya mashinikizo haya."

3807555

captcha