IQNA

IUMS: Tawala za Saudia, UAE zimehusika na kifo cha Mursi

19:38 - June 18, 2019
Habari ID: 3472006
TEHRAN (IQNA) – Mwenyekiti wa Jumyuiya ya Kimataifa ya Maulamaa Waislamu (IUMS) amezituhumu tawala za Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kuwa zimehusika katika kifo cha rais wa zamani wa Misri Muhammad Mursi.

Katika taarifa Jumanne, Sheikh Ahmad al Raysun, ametaja kifo cha Mursi kuwa ni fedheha kwa watawala wahaini wa Saudi Arabia ambao mikono yao imeroa damu ya watu wa Misri, Libya, Yemen, Sudan na mataifa mengine ya Waislamu.

Mwenyekiti wa Jumyuiya ya Kimataifa ya Maulamaa Waislamu  yenye makao yake Doha, Qatar aidha amesema kifo cha  Mursi ni fedheha kwa Chuo Kikuu cha Al Azhar na rais Abdel Fattah el Sisi wa Misri. Ameendelea kusema kuwa, Mursi ameteswa katika kipindi chote cha miaka sita ambayo amekuwa akishikiliwa korokoroni.

Mohammad Morsi, rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia Misri, ambaye aliondolewa madarakani kufuatia mapinduzi ya kijeshi yaliyoongozwa na rais wa sasa, Abdulfattah al-Sisi tarehe 3 mwezi Julai mwaka 2013, alifariki dunia Jumatatu wakati kesi iliyokuwa ikimkabili ikisikilizwa. Alizikwa Jumanne kimya kimya leo kimya kimya katika makaburi ya Medinat Nasr mashariki mwa Cairo, mji mkuu wa nchi hiyo.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imetoa mkono wa pole kwa familia ya Mohammed Morsi, kufuatia kifo tata cha rais huyo wa zamani wa Misri.

Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imeeleza kuwa, "Huku ikiheshimu mitazamo ya wananchi wa Misri, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inatoa mkono wa pole kwa familia, jamaa, marafiki, wafuasi na taifa la Misri kufuatia kifo cha Dakta Mohammad Morsi."

Wakati huo huo, Rais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki sambamba na kutoa mkono wa pole kwa familia na taifa la Misri kufuatia kifo hicho, amemtaja marehemu Morsi kama shahidi, huku akimtaja rais wa sasa wa Misri aliyemuondoa Morsi madarakani kupitia mapinduzi ya umwagaji damu, Abdel-Fattah el-Sissi, kama katili.

Katika hatua nyingine, Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS imempongeza Morsi na kumtaja kama shujaa, ambaye alisisimama kidete kuwatetea wananchi madhulumu wa Palestina hususan wanaoishi katika Ukanda wa Gaza.

Ofisi ya Kamishna mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa imesema ni matumaini yake kuwa uchunguzi huru na wa kina utafanyika juu ya mazingira ya kifo cha Rais wa zamani wa Misri, Mohamed Morsi kilichotokea jana wakati akiwa mahakamani.

Msemaji wa ofisi hiyo, Rupert Colville amesema hayo kupitia taarifa iliyotolewa mjini Geneva Uswisi, baada ya ripoti ya kwamba siku ya Jumatatu na kubaini, kuwa rais huyo wa zamani alikuwa korokoroni chini ya mamlaka za Misri wakati wa kifo chake, serikali inawajibu wa kuhakikisha kuwa alitendewa kiutu na kwamba haki yake ya uhai na afya ziliheshimiwa.

Amesema kifo chochote cha ghafla wakati mtu yuko rumande kinapaswa kufuatiwa na uchunguzi wa haraka, wa kina na huru na ulio wazi ambao utafanywa na chombo kilicho huru ili kubainisha sababu za kifo.

Murs, mwanachama wa Harakati ya Ikwanul Muslimin, alichaguliwa kuwa rais mwaka Juni 2012 baada ya kupinduliwa utawala wa dikteta Husni Mubarak lakini akaondolewa katika mapinduzi ya jeshi. Mwaka mmoja baadaye Morsi alishahukumiwa kifungo cha maisha jela kwa mashtaka yanayohusu ugaidi.

Mursi alizaliwa katika kijiji cha El-Awwadh katika jimbo lililopo kwenye delta za mto Nile la Sharqiya mwaka 1951.

Alisomea Uhandisi katika chuo Kikuu cha Cairo katika miaka ya 70 kabla ya kuhamia nchini Marekani ambapo alitunukiwa Shahada ya Uzamivu (PhD) katika Uhandisi.

Morsi aliweka rekodi ya kuwa kiongozi wa kwanza kuchaguliwa katika uchaguzi wa haki na huru mwaka 2012, akiwa kiongozi mwandamizi harakati ya Kiislamu ya Ikanul Muslimin ambayo imepigwa marufuku kwa sasa nchini humo.

3820368

captcha