Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, mwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameibuka wa tatu katika mashindano hayo yaliyofanyika Tehran ambapo nafasi ya kwanza ilishikwa na Hakima Nasiri wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran akifuatiwa na Aqila Ben Qrush wa Algeria.
Mashindano hayo maalumu ya wanawake yalikuwa na washiriki 28 waliohifadhi Qur’ani kikamilifu kutoka nchi 28 ambao ambapo kuli jopo la majaji ni wataalamu 9 wa Qur’ani kutoka Iran na wengine watano kutoka nchi za kigeni.
Bi. Ashura Amani Lilanga mwenye umri wa miaka 18 ameandamana na baba yake katika mashindano hayo ya Tehran. Katika mahojiano na mwandishi wa IQNA, amesema: “Kabla ya kushiriki katika mashindano haya, niliwahi kushiriki katika mashindano ya kimataifa nchini Jordan lakini sikuwa miongoni mwa washindi.” Anaongeza kuwa: “Mashindano ya Iran ni bora kuliko ya Jordan kwani hapa washiriki wamepokelewa kwa ukarimu mkubwa.”
Binti huyo Mtanzania aliyehifadhi Qur’ani Tukufu kikamilifu anasema: “Familia yangu imekuwa na mchango mkubwa katika kunisaidia kuhifadhi Qur’ani Tukufu.” Anaendelea kusema, “katika familia yetu yenye watoto sita wa kike na wawili wa kiume na ni mimi pekee niliyehifadhi Qur’ani Tukufu.”
Bi. Amani Lilanga anasema nchini Tanzania hakuna mashindano ya kitaifa ya kuhifadhi Qur’ani ya wanawake lakini hufanyika mashindano ya kieneo. Anaongeza kuwa alifanikiwa kuhifadhi Qur’ani kikamilifu baada ya jitihada ya miaka sita. Aidha anasema nchini Tanzania suala la kuhifadhi Qur’ani hupewa umuhimu mkubwa miongoni mwa Waislamu.
Mashindano ya 35 ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu ya Iran mwaka huu yalifunguliwa rasmi Jumatano 19 Aprili na kukamilika baada ya wiki moja Jumatano 25 Aprili. Mashindano hayo yalijumuisha yale ya ya kawaida maalumu kwa ajili ya wanaume, na pia kulikuwa na mashindano mengine ya Qur'ani ya wanawake, ya wenye ulemavu wa macho, ya wanafunzi wa vyuo vikuu na ya wanachuo wa vyuo vya kidini.
Mashindano ya Kimataifa ya Qur'ani ya Iran, ambayo yanafanyika katika miji mitatu ya Tehran, Mashhad na Qum, ni tukio kubwa zaidi linalohusiana na Qur'ani katika Ulimwengu wa Kiislamu na yamekuwa yakiimarika kila mwaka.
Mashindano hayo ya kimataifa ya Qur'ani yamefanyika kwa kaulimbiu ya "Kitabu Kimoja, Umma Mmoja" na yalizinduliwa sambamba na kuanza mwezi huu mtukufu wa Shaaban uliojaa fadhila.