IQNA

Aliyechochea mauaji ya Waislamu Uingereza afungwa miaka 12

19:26 - September 04, 2019
Habari ID: 3472114
TEHRAN (IQNA)- Mzungu mbaguzi mwenye kufuatia itikadi ya wale wanaoamini wazungu ndio wanadamu bora zaidi duniani, amefungwa jela miaka 12 nchini Uingereza baada ya kupatikana na hatia ya kuchochea mauaji ya Waislamu.

David Parnham, ambaye binafsi alijipachika lakabu ya 'Muuaji wa Waislamu', na kutuma vifurushi vilivyokuwa na kemikali bandia ya anthrax atahudumu kifungo katika hospitali na akipona atapelekezwa gerezani.

Mahakama ya Old Bailey mjini London imesikia namna mtuhumiwa huyo, 36, alivyotuma barua za kichochezi katika misikiti, Malkia Elizabeht na wanasiasa David Cameron na Theresa May.

Mbaguzi huyo mashuhuri wa rangi wa Uingereza amekiri kwamba amekuwa akiwachochea raia wa nchi hiyo kuwashambulia Waislamu.

David Parnham amekiri mahakamani kwamba, alikuwa akiwaandika barua na jumbe nyingi wakazi wa London, Midlands na Yorkshire akiwataka kushambulia misikiti na vituo vya Kiislamu tarehe 3 Aprili mwaka huu wa 2018.

Barua hizo zilitenga alama kwa ajili ya watu watakaowashambulia Waislamu kama vile alama kumi kwa mashambulizi ya maneno, alama 50 kwa kuwamwagia Waislamu tindikali usoni, alama 1,000 kwa mtu atayeshambulia misikiti ya Waislamu kwa bomu na alama 2,500 kwa mtu atakayeshambulia mji mtakatifu wa Makka.

Kwa kipindi cha miaka miwili pia David Parnham alikuwa akituma paketi zenye poda nyeupe kwa wawakishi Waislamu wa Uingereza, wanasiasa mashuhuri na kwenye vituo vya Kiislamu nchini Uingereza ili kuwatia woga na hofu.

Polisi ya Uingereza imesema kwamba, David Parnham ni mwanachama wa kundi la wabaguzi linalojulikana kwa jina la Dylann Roof linalomuenzi mbaguzi mashuhuri wa kizungu aliyekuwa na jina hilo ambaye aliwaua Wamarekani 9 wenye asili ya Afrika katika kanisa moja huko kusini mwa California.   

3469333

captcha