IQNA

Bahrain yawakandamiza wanazuoni wa Kishia kabla ya Ashura

17:24 - September 07, 2019
Habari ID: 3472118
TEHRAN (IQNA) - Utawala wa kiimla wa Bahrain umeanzisha wimbi jipya la kuwakandamiza wanazuoni wa Kiislamu wa madhehebu ya Shia katika mwezi huu wa Muharram.

Taarifa zinasema utawala wa ukoo wa Aal Khalifa nchini Bahrain umewaita na kuwasaili wanazuoni kadhaa wakiwemo Seyed Jaber al-Shahrakani, Sheikh Mohammad Ali al-Mahfuz, Sheikh Mohammad A’ashur, na Sheikh Zoheir al-Khal.

Muharram ni mwezi wa kwanza katika kalenda ya Kiislamu ya Hijria Qamaria. Waislamu wa madhehebu ya Shia na wengine kote duniani hujumuika katika siku 10 za kwanza za Muharram kuomboleza kuuawa shahidi mjukuu wa Mtume Muhammad SAW, Imam Hussein AS pamoja na wafuasi wake watiifu.

Taarifa zinasema wanazuioni kadhaa tayari wametiwa mbaroani na hadi sasa waliobainika kukamatwa ni Sheikh Menbar al-Ma’atouq na Sheikh Mohammad al-A’ajimi.

Aidha wakuu wa utaala wa Aal Khalifa wamewazuia Waislamu katika maeneo kadhaa kupandisha bendera ambazo hutumika katika maombolezo ya siku 10 za Muharram.

Tangu Februari mwaka 2011, wakati ulipoanza mwamko wa Kiisamu Asia Magharibi, Bahrain imekuwa uwanja wa maandamano ya amani ya wananchi wanaopinga utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa.

Wananchi hao wanataka kuwepo uhuru, utekelezwe uadilifu, ukomeshwe ubaguzi na kuundwa serikali itakayochaguliwa na wananchi wenyewe.

Hata hivyo kwa msaada wa wanajeshi wa Saudi Arabia na askari usalama wa Imarati waliotumwa nchini Bahrain kupitia mpango wa ulinzi wa Ngao ya Kisiwa, utawala wa Aal Khalifa unatumia mkono wa chuma kukabiliana na matakwa ya wananchi hao.

Kwa mujibu wa duru za haki za binadamu, Bahrain ina idadi kubwa zaidi ya wafungwa wa kisiasa kulinganisha na idadi ya watu katika nchi hiyo ndogo zaidi katika Ghuba ya Uajemi.

3469341

captcha