IQNA

Ujumbe wa Rais Putin kwa Mkutano wa Russia na Ulimwengu wa Kiislamu

20:48 - November 29, 2019
Habari ID: 3472241
TEHRAN (IQNA) – Rais Vladimir Putin wa Russia ametoa wito kwa kuwepo jitihada za pamoja baina ya Russia na Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC) katika kukabiliana na changamoto za kimataifa.

Rais Putin ameyasema hayo Ijumaa katika ujumbe wake uliosomwa katika mkutano wa ‘Kundi la Maono ya Kistratijia ya Russia na Ulimwengu wa Kiislamu’ ambao unafanyika katika mji wa Ufa katika Jamhuri ya Bashkorostan nchini Russia.

Katika ujumbe huo ambao umesomwa na Rais wa Jamhuri ya Tatarstan ya Russia Rustam Minnikhanov, Rais Putin amesema mkutano huo utapelekea kuimarishwa uhusiano wa Moscow na OIC kwa msingi wa kuaminiana.

“Ni matumaini yangu kuwa, mtakuwa na mazungumzo marefu ambapo fikra zenu zitapelekea kuimarisha hali ya kuaminiana na maelewano baina ya nchi zetu na pia watu wetu,” amesema rais wa Russia katika ujumbe wake.

Kwa mujibu wa Putin, washiriki katika kikao hicho pia wanabadilishana mawazo kuhusu kuimarisha mazungumzo baina ya dini mbali mbali.  Ameongeza kuwa, Russia na nchi za OIC zinafungamana katika kuheshimu sheria za kimataifa, mfumo wa demokrasia duniani na pia zina azma ya kuhakikisha kuna amani na usalama duniani.

“La muhimu zaidi ni kuwa Russia na OIC ziratibu kwa pamoja jitihada zao katika kukabiliana na vitisho pamoja na changamoto duniani, utatuzi wa migogoro wa kieneo na masuala ya kibinadamu,” amesisitiza rais Putin.

Mkutano wa ‘Kundi la Maono ya Kistratijia ya Russia na Ulimwengu wa Kiislamu’ ulianza Alhamisi 18 na unamalizika Jumamosi 30 Novemba. Russia ilijiunga na Jumuiya ya Nchi za Kiislamu mwaka 2006 kama mwanachama mwangalizi na tokea wakati huo kumekuwa kukifanyika mikutano baina ya pande mbili hizo. Idadi ya Waislamu nchini Russia sasa imefika watu milioni 25 kati ya watu milioni 145 nchini humo.

Aghalabu ya Waislamu wa Russia wanafuata madhehebu ya Hanafi lakini pia kuna Masunni wa Madhehebu ya Shafi na pia kuna Waisalamu wa madhehebu ya Mashia.

Aghalabu ya Waislamu nchini Russia wanaishi katika mji mkuu Moscow na miji mingine mikubwa kama vile St. Petersburg and Yekaterinburg. 

3860335

captcha