IQNA

Mkuu wa Shirika la Hija la Iran yuko Saudia kufuatia mwaliko wa Waziri wa Hija

11:23 - December 08, 2019
Habari ID: 3472261
TEHRAN (IQNA) - Mkuu wa Shirika la Hija na Ziyara la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran leo ameelekea Saudi Arabia kufuatia mwaliko rasmi wa Waziri wa Hija na Umrah wa nchi hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa, Ali Reza Rashidian, Mkuu wa Shirika la Hija na Ziyara la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema: "Safari hii ni kwa ajili ya kufanya mazungumzo kuhusu Hija ya mwaka ujao na inafuatia mwaliko rasmi wa Waziri wa Hija na Umrah wa Saudia Arabia."

Rashidian ameelezea matumaini yake kuwa katika safari hiyo ataweza kufanya mazungumzo na wakuu wa Saudia kuhusu kuandaliwa ibada ya Hija yenye heshima, taadhima, usalama na utulivu kwa Mahujaji kutoka maeneo yote ya dunia. Katika Hija ya mwaka uliopita, Wairani 86,550 walifanikiwa kutekekeleza ibada hiyo muhimu.

Akizungumza Julai tatu mwaka huu wakati alipokutana na wasimamizi wa Hija hapa Iran, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu alisema: "Serikali ya  Saudi Arabia ina jukumu zito la kudhamini usalama wa Mahujaji sambamba na kulinda heshima yao."

Katika kikao hicho ambacho hufanyika kila mwaka kabla ya msafara wa kwanza wa Wairani wanaoelekea Hija, aliashiria masuala muhimu ya kisiasa yaliyomo kwenye ibada ya Hija kama kulindwa umoja, kuwatetea watu wanaodhulumiwa na kujitenga na washirikina na kusisitiza kuwa: “Umoja, kuwatetea wanaodhulumiwa kama taifa la Palestina na watu wa Yemen au kujitenga na kujiweka mbali na washirikina, yote hayo ni mambo ya kisiasa yanayooana na mafundisho ya Uislamu; na kwa msingi huo masuala ya kisiasa ya ibada ya Hija ni wajibu wa kidini na kiibada.“

3470055

captcha