IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Kuna haja ya kukabiliana na njama za kusahaulisha utamaduni wa jihadi na kufa shahidi

11:37 - December 27, 2019
Habari ID: 3472308
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, suala la kuwaenzi mashahidi ni jambo la lazima na ni jukumu la kila mtu kwani hivi sasa kuna siasa na harakati za kikhabithi zinazolenga kusahaulisha nembo za Mapinduzi ya Kiislamu hususan utamaduni wa jihadi na kuwa tayari kujitolea kufa shahidi katika njia ya Allah.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei amesema hayo wakati alipoonana na wajumbe wa kamati ya Kongamano la Mashahidi la mkoa wa Hormozgan wa kusini mwa Iran na huku akigusia historia ndefu ya jihadi na mapambano ya wananchi wa mkoa huo amesema kuwa, ushujaa na kusimama kwao imara katika njia ya haki  ni thamani na tunu zilizokita mizizi kwenye eneo hilo.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa, kila mtu anayekuwa tayari kufa shahidi katika njia ya haki ni nembo ya kujitolea na kuwa tayari kutoa kitu chake cha thamani sana yaani roho yake katika kupigania haki. 

Vile vile amesisitizia ulazima wa kutambulishwa na kuelimishwa vizuri vijana uwepo wa nembo na vigezo hivyo muhimu na vyenye thamani kubwa katika jamii zao na kuongeza kuwa, hivi sasa kuna njama maalumu za kuwarubuni watu wathamini nembo za ufisadi, kupenda dunia na mambo ya kipuuzi ili kuwasahaulisha vijana nembo zao zenye thamani kubwa za watu wanaojitolea kufa shahidi katika njia ya haki.

Miongozo hiyo iliyojaa busara ilitolewa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei tarehe 16 mwezi huu wa Disemba lakini imesambazwa Alkhamisi 27 Disemba kwenye kongamano hilo huko Bandar Abbas, kusini mwa Iran.

3866758

captcha