Sayyid Hassan Nasrullah amesema hayo jioni ya leo mjini Beirut Lebanon katika kumbukumbu maalumu ya kuuawa shahidi Kamanda Luteni Jenerali Qassem Soleimani pamoja na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu wa Mkuu wa Jeshi la Kujitolea la Wananchi wa Iraq maarufu kwa jina la Hashd al Shaabi waliouliwa kigaidi katika hujuma ya Marekani karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Baghdad Iraq, usiku wa kuamkia Ijumaa ya tarehe 3 Januari, 2020.
Katika hotuba yake iliyorushwa hewani mubashara na Televisheni ya Al Jazeera, Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon amesema, kuuliwa kigaidi Luteni Jenerali Soleimani akiwa pamoja na al Muhandis kumefanyika kwa amri ya moja kwa moja ya rais wa Marekani, Donald Trump ambaye naye amekiri kufanya jinai hiyo.
Amesema, ushindi wa kambi ya muqawama katika nchi za Syria, Lebanon, Palestina, Iraq, Yemen na pia suala la kukaribia uchaguzi nchini Marekani ni miongoni mwa sababu zilizoifanya Marekani itangaze hadharani kuhusika katika mauaji ya kigaidi ya Luteni Jenerali Qassem Soleimani.
Sayyid Nasrullah aidha amesema, kushindwa njama zote za Trump mbele ya Iran ni sababu nyingine muhimu ya kuuliwa kigaidi Kamanda Soleimani na kuongeza kuwa, lengo la Trump ni kuipindua Jamhuri ya Kiislamu ya Iran au kwa uchache kuipigisha magoti na kuilazimisha ikubali kuburuzwa na Marekani lakini ameshindwa kufikia lengo lake hilo. Vile vile amesema, hata kiatu cha Luteni Jenerali Soleimani kina thamani zaidi kuliko kichwa cha Donald Trump.