IQNA

Kombora la Ansarullah laangamiza Mamluki 60 wa Saudia nchini Yemen

12:36 - January 19, 2020
Habari ID: 3472387
TEHRAN (IQNA) - Makumi ya mamluki wa Saudi Arabia wameuawa katika operesheni iliyofanywa na jeshi la Yemen kwa kushirikiana na harakati ya Ansarullah huko kaskazini mwa Yemen.

Televisheni ya taifa ya Saudia jioni ya jana ilikiri kuwa mamluki zaidi ya 60 waliokuwa wakipigana kwa niaba ya Riyadh wameuawa katika shambulizi la kombora la Ansarullah lililolenga kambi ya kijeshi ya muungano huo vamizi unaoongozwa na Saudia katika mkoa wa Ma’rib wa kaskazini mwa nchi.

Duru za hospitali zimearifu kuwa, wanajeshi 45 wa muungano huo vamizi ni miongoni mwa waliouawa katika shambulio hilo la jana ya Ansarullah, ambayo inatajwa kuwa kubwa zaidi katika wiki za hivi karibuni.

Mapema jana Jumamosi pia, mamluki wengine 12 wa muungano huo wa kijeshi wa Saudia na Imarati huko nchini Yemen waliangamizwa katika operesheni ya wanamapambano wa Ansarullah, katika mkoa wa Hajjah, kaskazini magharibi mwa nchi hiyo maskini ya Kiarabu.

Inafaa kuashiria kuwa, Saudia ilianzisha mashambulizi dhidi ya Yemen mwishoni mwa mwezi Machi 2015 kwa lengo la kuiondoa madarakani Harakati ya Ansarullah na kumrejesha usukani Abdrabbuh Mansour Hadi, rais wa zamani wa nchi hiyo aliyejiuzulu na kukimbilia Riyadh.

Hata hivyo Saudi Arabia na washirika wake wameshindwa kufikia malengo yao hayo huku wakisababisha maafa makubwa ya kibinadamu ikiwa ni pamoja na kuwaua raia wasio na hatia. Zaidi ya watu 16,000 wanaripotiwa kupoteza maisha katika vita vya Saudia dhidi ya Yemen. Idadi kubwa ya watoto na wanawake ni miongoni mwa waliopoteza maisha moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja kutokana na vita dhidi ya Yemen vinavyoongozwa na Saudia kwa himaya ya madola ya Magharibi hasa Marekani na utawala haramu wa Israel.

3872525/

captcha