IQNA

Magaidi wakufurishaji wa Boko Haram waua watu watatu nje ya msikiti Nigeria

13:41 - January 27, 2020
Habari ID: 3472410
TEHRAN (IQNA) – Magaidi wakufurishaji wa kundi la Boko Haram wameua Waisalmu watatu na kuwajeruhi wengine 13 katika hujuma iliyotekelezwa nje ya msikiti katika mjini Gowza, jimboni Borno kaskazini mashariki wa nchi hiyo.

Taarifa zinasema tukio hilo limejiri wakati wa Sala yay a Alfajiri katika mtaa wa Bulabulin ulio eneo la kusini wa jimbo hilo.

Maafisa wa usalama wamesema hujuma hiyo imetekelezwa na magaidi wawili wa kike waliokuwa wamejifunga mishipi ya mabomu na walijilipua kabla ya kuingia msikitini ambapo nao pia waliangamia papo hapo.

Waislamu wa kaskazini mashariki mwa Nigeria wamekuwa wakilengwa kwa muda mrefu na magaidi wakufurishaji wa Boko Haram ambao huwakufurisha Waislamu wote wasiokubaliana  itikadi zao potovu. Misikiti na shule za Waislamu wasioafikiana na Boko Haran hulengwa mara kwa mara na kundi hilo la kigaidi.

Neno Boko Haram kwa ya lugha ya Kihausa, ambayo inatumiwa na aghalabu ya Waislamu wa Nigeria, lina maana ya 'elimu kutoka nchi za Magharibi ni haramu'.

Zaidi ya watu elfu 20 wamepoteza maisha nchini Nigeria tokea kundi la Boko Haram lianzishe uasi mwaka 2009 huku wengine zaidi ya milioni mbili wakilazimika kukimbia makazi yao kutokana na ugaidi wa Boko Haram ambao sasa umeenea katika nchi jirani kama vile Cameroon, Niger na Chad. Halikadhalika ugaidi huo wa Boko Haram umepelekea Waislamu wa kaskazini mwa Nigeria kubakia nyuma kimaendeleo na hivyo kuathiri vibaya mustakabali wao. Serikali ya Nigeria pia inalaumiwa kwa kuzembea katika kukabiliana namagaidi hao huku kukiwa na ripoti kuwa baadhi ya majenerali jeshini na maafisa wa serikali wanaofaidika na ugaidi huo wa Boko Haram.

3470457

captcha