IQNA

Katika barua maalumu

Spika wa Bunge la Iran ataka mabunge ya nchi za Kiislamu yapinge 'Muamala wa Karne'

21:34 - January 29, 2020
Habari ID: 3472418
TEHRAN (IQNA) - Spika wa Bunge la Iran (Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu) ametoa wito wa kukabiliana na mpango bandia wa Rais Donald Trump uliopewa jina la "Muamala wa Karne". Aidha ametoa wito kutatuliwa mgogoro wa Palestina kwa kutumia njia ya kura ya maoni na udiplomasia wa kibunge.

Katika barua yake aliyowatumia maspika wa mabunge ya nchi za Kiislamu, Dakta Ali Larijani ametangaza kuchukizwa kwake na hatua ya Rais Donald Trump wa Marekani ya kuzindua mpango bandia eti wa "Muamala wa Karne" na amesisitiza udharura wa kukabiliana na mpango huo na kutatuliwa mgogoro wa Palestina.

Larijani amesema kuzinduliwa kwa mpango huo kunakiuka makubaliano yote, sheria za kimataifa, hati ya Umoja wa Mataifa, Jumuiya ya Nchi za Kiarabu na Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu kuhusu kadhia ya Palestina na kuongeza kuwa: Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imetoa pendekezo la kidemokrasia na kisiasa la kuitishwa kura ya maoni katika ardhi zote zinazokaliwa kwa mabavu kwa kuwashirikisha wakazi wake asili chini ya usimamizi wsa Umoja wa Mataifa, na inakutambua kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa sasa na kutatuliwa kwa njia za kiadilifu kadhia ya Palestina kuwa ni haki ya taifa linalodhulumiwa la Palestina.

Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu amewataka maspika wenzake wa nchi za Kiislamu kufanya jitihada kubwa za kukabiliana na mpango bandia wa "Muamala wa Karne" na kusaidia zaidi mchakato wa kutafuta suluhisho la mgogoro wa Palestina kwa kuunga mkono pendekezo la kuitishwa kura ya maoni na kutumia udiplomasia wa kibunge.

Itakumbukwa kuwa Jumanne ya jana Rais Donald Trump wa Marekani alizundua mpango wa Muamala wa Karne kwa ajili ya kile alichokiita utatuzi wa mgogoro wa Palestina ambao umepingwa na jamii kubwa ya kimataifa.

Mpango huo wa Marekani ambao unautambua mji mtakatifu wa Quds kuwa mji mkuu wa utawala bandia wa Israel na kupuuza moja kwa moja haki za kimsingi za wakaazi asilia wa mji huo, unathibitisha wazi kuwa umebuniwa kwa madhumuni ya kulinda maslahi haramu ya utawala huo na kudhamini usalama wake unaolegalega.

Usaliti wa baadhi ya nchi vibaraka za Kiarabu ulidhihirika wazi wakati wa kuzinduliwa mpango huo eti wa 'Muamala wa Karne' unaokanyaga na kusaliti wazi wazi malengo matukufu ya taifa la Palestina. Mabalozi wan chi za Kiarabu za Oman, Umoja wa Falme za Kiarabu waliandamana na mtawala wa Marekani katika uzinduzi wa mpango huo unaolisaliti taifa la Palestina.

Iwe ni kwa kujua au kutojua, Waarabu hao vibaraka wanashirikiana wazi na Marekani pamoja na utawala wa kibaguzi wa Israel katika kusahaulisha Palestina na Quds Tukufu, ambalo ni suala la kwanza kipaumbele katika ulimwengu wa Kiislamu na wakati huo huo kuwavua silaha wanamapambano wa Kiislamu wa Paletina.

3875150

captcha