IQNA

Rais Abbas katika Baraza la Usalama: Muamala wa Karne ni wa kibaguzi

17:11 - February 12, 2020
Habari ID: 3472464
TEHRAN (IQNA) - Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina ameliambia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa, mbali na mpango wa Rais Donald Trump wa Marekani uliopewa jina la Muamala wa Karne kukanyaga maazimio ya umoja huo, pia ni wa kibaguzi na unakiuka mamlaka na uhuru wa kujitawala Palestina.

Akizungumza Jumanne, Mahmoud Abbas amebainisha kuwa, mpango huo kama ilivyokuwa mipango mingine iliyojaa njama dhidi ya Wapalestina nao utafeli na kugonga mwamba. Ameutaja mpango huo wa Kimarekani-Kizayuni kama zawadi ya Trump kwa Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala khabithi wa Israel.

Aidha Mahmoud Abbas ameeleza kuwa, Quds Tukufu na ardhi za Palestina sio bidhaa ya kuuza kwa hivyo Muamala wa Karne hautotekelezwa.

Ameeleza bayana kuwa, "Mpango huo uliozinduliwa Januari 28 na Rais wa Marekani, ni njama za Wazayuni na Wamarekani za kuzika katika kaburi la sahau kadhia ya Palestina." Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina ameongeza kuwa, mpango huo unapingwa na Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC) na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu (Arab League).

Tarehe 28 Januari, rais Donald Trump wa Marekani akiwa pamoja na waziri mkuu wa utawala bandia wa Israel, Benjamin Netanyahu alizindua mpango wa ubaguzi wa kimbari wa Muamala wa Karne.

Kuitambua rasmi Quds (Jerusalem) kuwa mji mkuu wa utawala wa Kizayuni, kuupatia utawala huo haramu umiliki wa asilimi 30 ya eneo la Ufukwe wa Magharibi wa Mto Jordan, kupingwa haki ya wakimbizi wa Kipalestina kurejea nchini kwao na kupokonywa silaha kikamilifu ile itakayoitwa nchi ya Palestina ni miongoni mwa vipengele vya mpango huo wa udhalilishaji.

3878238

captcha