IQNA

Sayyed Hassan Nasrallah

Jasusi Al-Fakhoury aliachiliwa kufuatia mashinikizo ya Marekani

19:09 - March 21, 2020
Habari ID: 3472586
TEHRAN (IQNA) - Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon amesema, maadui wanafanya kila njia ili kuyumbisha imani iliyopo baina ya Muqawama na wananchi, ambao ndio watoaji msukumo halisi kwa mhimili wa muqawama.

Sayyid Hassan Nasrallah ameyasema hayo katika hotuba aliyotoa Ijumaa usiku kupitia televisehni ya Al Manar kuhusiana na matukio ya Lebanon na eneo.

Katibu Mkuu wa Hizbullah ameashiria kadhia ya kuachiwa huru jasusi wa Kimarekani na Kizayuni Amer Al-Fakhoury na kueleza kwamba, misimamo ya Hizbullah kuhusu kadhia hiyo inatokana na msimamo wa wananchi na kwamba kuna uvumi na kauli za uongo zinazotolewa juu ya suala hilo.

Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Sayyid Hassan Nasrallah amezungumzia uingiliaji na utoaji vitisho wa Marekani kuhusiana na kuwekwa kizuizini al-Fakhoury na akabainisha kwamba, tangu kibaraka huyo alipotiwa nguvuni miezi sita nyuma, Marekani ilianza kutoa vitisho na mashinikizo kwa serikali ya Lebanon ili aachiliwe huru.

Katibu Mkuu wa Hizbullah amesema: Marekani ilitoa vitisho vikali na vya moja kwa moja kwa baadhi ya shakhsia wa kisiasa na wa serikali ya Lebanon kwamba itawawekea vikwazo endapo al-Fakhoury hatatolewa hatiani na kuachiwa huru.

Ametahadharisha kwa kusema, ni hatua hatari iliyochukuliwa ya kusalimu amri kwa mashinikizo ya Marekani katika kadhia hiyo, kwa sababu itaandaa mazingira ya uingiliaji mkubwa zaidi wa Marekani katika siku za usoni.

Amer al-Fakhoury ambaye ana uraiapacha wa Lebanon na Marekani alitiwa nguvuni Septemba 2019 baada ya kurejea Lebanon akitokea Marekani. Wakati Lebanon ilipoavmiwa na kukaliwa kwa mabavu, jasusi na kibaraka huyo wa Kizayuni na Kimarekani alikuwa kamanda wa jeshi katika jela ya al-Khiyam, kusini mwa Lebanon na alikuwa akishirikiana na utawala wa Kizayuni wa Israel.

Kwa mashinikizo ya Marekani na kwa kutumia utetezi wa kimaonyesho uliotolewa na mawakili wa Amer al Fakhoury waliodai kwamba mashtaka dhidi ya mteja wao yamechukua muda mrefu, tarehe 16 Machi, mahakamna ya kijeshi ya Lebanon ilitoa hukumu ya kuachiwa huru kibaraka huyo, ambaye ni maarufu kama "chinjachinja wa mahabusu ya al-Khiyam" aliyekuwa akiufanyia ujasusi pia utawala wa Kizayuni.

Wananchi wa Lebanon walilalamikia vikali uingiliaji wa Marekani kwa kukusanyika mbele ya mahakama ya kijeshi; na hata baadhi yao wakachoma moto matairi na kufunga baadhi ya barabara kuu.

3886688

captcha