Guterres ametoa wito huo kwa njia ya video na kusema kuwa mwezi wa Ramadhani wa mwaka huu unatofautiana sana na miaka mingine kwa kuwa shughuli nyingi za kijamii zitaathiriwa na maambukizi ya virusi vya Corona na kwamba akthari ya wakazi wa maeneo yenye mapigano kwa mara nyingine watakumbwa na huzuni ndani ya mwezi huu kutokana na vita na ukosefu wa usalama katika pande zote. Sambamba na kuwatakia kila la kheri Waislamu diniani, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amekariri kwa mara nyingine wito wake alioutoa tarehe 23 Machi mwaka huu juu ya kusitishwa haraka vita na mapigano duniani.
António Guterres amesema: "Mimi ninakariri ombi langu kwa mara nyingine kwa kuashiria aya ya Qur'an Tukufu inayosema , 'Na wakielekea amani nawe pia elekea, na mtegemee Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ndiye Mwenye kusikia Mwenye kujua.' Sura ya 8 aya ya 61."
Akizungumzia juu ya uungaji mkono wa matabaka ya watu waliopata madhara, sambamba na kutoa shukurani kwa serikali na wananchi katika ulimwengu wote wa Kiislamu amesisitiza kuwa, watu wengi duniani wamekuwa wakihitajia misaada hata kabla ya kuibuka janga la corona. Wito huo umetolewa katika hali ambayo nchi za Yemen, Syria na Iraq bado zinakabiliwa na uingiliaji wa kijeshi wa makundi yaliyoratibiwa ya kigaidi yanayoungwa mkono na Marekani na baadhi ya nchi za Kiarabu na Magharibi.