IQNA

Msikiti wa Paris, Ufaransa kufunguliwa kuanzia Jumanne

0:04 - May 31, 2020
Habari ID: 3472819
TEHRAN (IQNA) – Msikiti mkubwa zaidi katika mji mkuu wa Ufaransa, Paris, utafunguliwa tena Jumanne.

Kwa mujibu wa kamati ya msikiti huo ambao Kifaransa unajulikana kama La Grande Mosquée de Paris, waumini wataruhusiwa kuingia katika eneo hilo la ibada kwa sharti la kuzingatia taratibu na kanuni za kiafya za kuzuia kuenea ugonjwa wa COVID-19.

Kati ya masharti ya kuzingatiwa ni kuvaa maski au barakoa, kutokaribiana waumini na kushika wudhuu nyumbani na si msikitini. Aidha Bodi ya La Grande Mosquée de Paris imesema waumini wenye umri wa zaidi ya miaka 65 wametakiwa wasifike msikitini kwani wanakabiliwa na hatari kubwa zaidi ya kuambukizwa COVID-19.

Msikiti huo wa Paris ulifungwa kwa muda mwezi Machi ili kuzuia kuenea ugongjwa ambukizi wa COVID-19.

La Grande Mosquée de Paris ambao ni maarufu kama Msikiti wa Paris au Msikiti wa Jamia wa Paris uko katika mtaa wa  5th arrondissement na kati ya misikiti mikubwa zaidi Ufaransa.

Hadi kufikia Mei 30, watu 151,000 walikuwa wameambukizwa COVID-19 nchini Ufaransa na miongoni mwao 68,268 wamepona na 28,771 wamepoteza maisha.  Wakuu wa Ufaransa sasa wameanza kuondoa zuio la watu kutoka nje baada ya kudhibiti maambukizi ya ugonjwa huo.

3901900

captcha