IQNA

Walowezi wa Kizayuni wauhujumu Msikiti wa Al Aqsa

11:40 - July 31, 2020
Habari ID: 3473017
TEHRAN (IQNA) - Vijana wa Kipalestina wamekabiliana na walowezi wa Kizayuni waliokuwa wakifanya juhudi za kuvamia na kuingia katika Msikiti wa al-Aqswa.

Taarifa kutoka Quds inayokaliwa kkwa mabavu zinasema kuwa, kundi la walowezi wa Kizayuni lilikuwa na nia ya kuvamia na kuingia katika Msikiti wa al-Aqswa ambapo vijana wa Kipalestina walikabiliana na walowezi hao kuwazuia kuingia katika msikiti huo mtakatifu.

Hivi karibuni makumi ya walowezi wa Kizayuni waliuvamia tena Msikiti wa al-Aqswa huko Palestina wakisaidiwa na askari wa jeshi la utawala haramu wa Israel na kuuvunjia heshima msikiti huo ambao ni kibla cha kwanza cha Waislamu.

Vitendo vya kuyavunjia heshima matukufu ya Kiislamu vinafanyika katika hali ambayo, viongozi wa nchi za Kiarabu na jamii ya kimataifa wameendelea kunyamaza kimya na kutochukua hatua zozote za kukabiliana na vitendo hivyo.

Katika miaka ya hivi karibuni, utawala wa Kizayuni wa Israel umeshadidisha hujuma na uvamizi wake dhidi ya maeneo ya Wapalestina ukifanya njama za kufikia malengo yake haramu katika ardhi za Wapalestina.

Msikiti wa al-Aqswa ambao ni kibla cha kwanza cha Waislamu umekuwa ukiandamwa na njama mtawalia za utawala vamizi wa Israel, hatua ambazo zinakwenda sambamba na ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika maeneo ya Wapalestina.

3472139

captcha