IQNA

Marufuku ya kuingia Karbala wakati wa Muharram kutekelezwa

15:38 - August 24, 2020
Habari ID: 3473099
TEHRAN (IQNA) –Idara ya Polisi katika jimbo la Karbala nchini Iraq imetangaza kuwa ni marufuku kwa watu wasio wakaazi kuingia katika jimbo hilo hadi tarehe 13 Muharram inayosadifiana na 2 Septemba.

Katika taarifa msemaji wa Idara ya Polisi Ala Al-Ghanemi amesema uamuzi huo ni kwa mujibu wa ushauri wa wataalamu wanaokabiliana na janga la COVID-19.

Aidha amesema mijimuiko ya aina yoyote ni marufuku wakati huu ili kuzuia kuenea ugonjwa wa COVID-19

Kila mwaka, katika siku zinazoelekea Ashura, siku aliyouawa shahidi mjukuu wa Mtume Muhammad SAW, Imam Hussein AS, mamilioni ya wafanya ziara hufika katika mji wa Karbala katika haram Takatifu za Imam Hussein AS na Hadhrat Abbas AS kwa ajili ya kuomboleza kuuawa shahidi wawili hao.

Imam Husain AS akiwa na wafuasi wake watiifu 72 waliuawa shahidi kikatili na kinyama mwaka wa 61 Hijria, yaani miaka 1381 iliyopita, katika jangwa la Karbala, Iraq ya leo, katika mapambano ya kishujaa ya ushindi wa damu mbele ya upanga.

Vita vya Karbala vilikuwa moja kati ya vita mashuhuri katika historia ya Kiislamu na ya mwanadamu, vilitokea baina ya majeshi ya haki na batili katika ardhi ya Karbala huko Iraq. Siku hii inajulikana kwa jina la Ashura. 

3918502

captcha