IQNA

Msikiti mmoja Ufaransa wapokea vitisho

12:36 - October 28, 2020
Habari ID: 3473304
TEHRAN (IQNA) – Msikiti mmoja katika wilaya ya Vernon kaskazini mwa Ufaransa umepokea vitisho vya kushambuliwa huku chuki dhidi ya Uislamu ikishadidi nchini humo.

Ujumbe uliotumwa katika sanduku la barua la msikiti huo ulikuwa na vitisho vya mauaji na matusi dhidi ya Waturuki, Waarabu na wale wote ambao huswali katika msikiti huo mara kwa mara.

"Vita vimeanza. Tutakutimueni kutoka katika nchi yetu. Mtawajibishwa kufuatia kifo cha Samuel," ujumbe huo ulisema.

Ujumbe huo ulikuwa ukimuashiria Samuel Paty, mwalimu katika Chuo cha Bois-d'Aulne katika kitongoji cha Paris cha Conflans-Sainte-Honorine ambaye aliuawa kwa kukatwa kichwa na Abdullakh Anzorov mnamo Oktoba 16. Anzorov aliyekuwa na umri wa miaka 18 na mwenye asili ya Chechnia alikasirishwa na kitendo cha Samuel kuonysha katuni zinazomvunjia heshima Mtume Muhammad SAW darasani katika moja ya masomo ya uhuru wa maoni. Anzorov aliuawa katika oparesheni ya polisi punde baada ya kumkata kichwa Samuel.

Tiship dhidi ya msikiti huo pia limejumuisha matusi dhidi ya wanawake Waislamu wanaovaa Hijabu.

Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa amewakasirisha Waislamu zaidi baada ya kuunga mkono uchapishwaji wa katuni zinazomvunjia heshima Mtume Muhammad SAW huku akidai kuwa eti Uislamu ni dini inayokumbwa na mgogoro duniani.

Tamko hilo la Macron limechochea zaidi chuki dhidi ya Uislamu na kupelekea Waislamu kuishi kwa hofu ya kushambuliwa. Aidha hivi sasa kumeanzishwa kampeni ya kususia bidhaa za Ufaransa imeanza kote duniani kulalamikia hatua ya wakuu wa nchi hiyo kuchochea chuki dhidi ya Uislamu au Islamophobia.

3472960

 

captcha