IQNA

Kiongozi wa Ansarullah

Macron anatumiwa na Wazayuni kuutusi na kuuvunjia heshima Uislamu

14:36 - October 30, 2020
Habari ID: 3473309
TEHRAN (IQNA)-Katibu Mkuu wa Harakati ya Ansarullah ya Yemen amesema rais Emmanuel Macron wa Ufaranmsa ni kikaragosi kinachochezeshwa na Wazayuni kichukue hatua za kuutusi na kuuvunjia heshima Uislamu.

Sayyid Abdulmalik Badruddin al-Houthi ameyasema hayo jana Alkhamisi katika hotuba aliyotoa katika mji mkuu wa Yemen, Sana'a kwa mnasaba wa maadhimisho ya Maulidi wa Bwana Mtume Muhammad SAW; na akaongeza kuwa umma wa Kiislamu unakabiliwa na matatizo na migogoro ambayo chanzo chake ni kujitenga na kujiweka mbali na mafundisho ya Mwenyezi Mungu.

Abdulmalik al-Houthi amesema, ni wajibu kwa Waislamu kukabiliana vikali na wanaomtusi na kumvunjia heshima Mtume SAW na akafafanua kuwa kukabiliana nao huko si kwa maana ya kuchukua hatua za kihalifu, bali inapasa kufanyike kwa kufuata usuli na misingi ya dini.

Katibu Mkuu wa Harakati ya Ansarullah ameuelezea utawala haramu wa Israel kuwa ni tishio kwa umma wa Kiislamu na uthabiti wa eneo la Asia Magharibi; na akabainisha kuwa, utawala wa Aal Saudi wa nchini Saudi Arabia, Imarati, utawala wa Aal Khalifa wa nchini Bahrain na utwala wa kijeshi wa Sudan ni washirika wa njama ya Marekani na Israel dhidi ya Ulimwengu wa Kiislamu.

Hivi karibuni  rais Emmanuel Macron wa Ufaransa alitoa matamshi ya kifidhuli na yasiyoendana na adabu za kidiplomasia wala misingi ya demokrasia ya Magharibi aliposisitiza kuwa serikali yake itaendelea kuruhusu kuchapishwa vikatuni vinavyomvunjia heshima Bwana Mtume Muhammad SAW.

Matamshi hayo ya Macron yamelaaniwa vikali katika Ulimwengu wa Kiislamu, ambapo moja ya matokeo ya kusambaa wimbi la ghadhabu katika mataifa ya Kiislamu ni kuanzishwa kampeni ya kususia bidhaa za Ufaransa katika mataifa hayo.

3472973

captcha