Katika mahojiano na Televisehni ya Al Jazeera, Macron ameonekana kubadili wazi wazi msimamo wake ulio dhidi ya Uislamu kwa kusema: "Nadiriki hisia za Waislamu kuhusu vibonzo vyenye kumvunja heshima Mtume Muhammad". Rais huyo wa Ufaransa ameendelea kujitetea kwa kusema kuwa, kuna watu pia ambao kwa vitendo vyao wanaupotosha Uislamu. Macron ameendelea kusema kuwa, vibonzo husika si mradi wa serikali na ni kazi ya gazeti ambalo halina uhusiano wowote na serikali.
Siku kadhaa zilizopota, Rais Macron wa Ufaransa alitangaza wazi wazi kuunga mkono jarida la Ufaransa ambalo lilichapisha vibonzo vyenye kumvunjia heshima Mtume Mtukufu wa Uislamu, Muhammad Al Mustafa SAW. Macron aidha alisema uchapishaji vya vibonzo hivyo utaendelea nchini humo.
Matamshi hayo ya Macron yamelaaniwa vikali na Waislamu kote duniani huku maandamano yakifanyika dhidi ya mtawala huyo wa Ufaransa. Nchi za Kiislamu kama vile Iran, Pakistan na Uturuki pia zimelalamikia rasmi matamshi hayo ya Ufaransa. Mashirika ya Ufaransa yanaripotiwa kuanza kupata hasara kubwa baada ya Waislamu kote duniani kuanzisha kampeni ya kutaka bidhaa za Ufaransa zisusiwe.
Licha ya kushadidi chuki dhidi ya Uislamu na kutetea vitendo vichafu vya kumvunjia heshima Bwana Mtume SAW kwa kisingizio cha uhuru wa kutoa maoni kunakofanywa na viongozi wa Ufaransa na baadhi ya viongozi wa Ulaya, lakini inaonekana kuwa, mbinu hii siyo tu kwamba haikubaliwi na shakhsia na watu huru ulimwenguni, bali ukweli ni kuwa, utendaji huu unafanyika kwa minajili ya kufunika na kuficha mambo na kujaribu kuhalalisha hatua na siasa zisizo na busara za Wamagharibi.