IQNA

Ufaransa yapiga marufuku taasisi inayopambana na chuki dhidi ya Uislamu

20:28 - November 20, 2020
Habari ID: 3473378
TEHRAN (IQNA)- Ikiwa ni katika kuendeleza kampeni dhidi asasi za Kiislamu, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ufaransa Gerald Darminian ametangaza mpango wa kupiga marufuku Taasisi ya Kupambana na Chuki Dhidi ya Uislamu au Islamophobia Ufaransa (CCIF).

CIIF ilianzishwa mwaka 2003 kama asasi isiyo ya kiserikali kwa lengo la kupambana na vitendo vya chuki dhidi ya Uislamu Ufaransa.

Katika taarifa siku ya Ijumaa Darmanin amesema taasisi hiyo ina muda wa siku nane kutoa maoni kuhusu uamuzi huo.

Kufuatia tangazo hilo, uongozi wa CCIF imesema hatua ya waziri huyo ni katika kutii wito wa mrengo wa kulia wenye misimamo mikali ya kufurutu ada. CIIF imesema sasa shughuli zake zitakuwa zinaendeshwa nje ya Ufaransa lakini itaendelea kutoa msaada wa kisheria kwa waathirika wa vitendo vya chuki dhidi ya Uislamu sambamba na kuziarifu taasisi za kimataifa kuhusu mkakati wa kukabiliana na ubaguzi Ufaransa.

Mwezi Oktoba, Drmanin alitangaza nia ya kupiga marufuku asasi kadhaa za Kiislamu zisizo za kisehrikali nchini humo.

Hayo yanajiri wakati ambao, matamshi ya hivi karibuni ya Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa kwamba Uislamu uko kwenye mgogoro duniani kote na msimamo wake wa kuunga makono kitendo kiovu cha jarida la nchi hiyo la Charlie Hebdo cha kuchapisha vikatuni vya kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW kimeughadhibisha Ulimwengu wa Kiislamu.

Maandamano makubwa yamefanyika na yanaendelea kufanyika katika nchi mbalimbali kulaani msimamo huo wa Macron. Mbali na maandamano, zinaendeshwa kampeni pia za kususia bidhaa za Ufaransa na sasa kampeni hiyo pia imeenea katika sekta za utamaduni.

3936295

captcha