IQNA

Saudia yatangaza kuunga mkono uhusiano na utawala wa Kizayuni

21:34 - November 22, 2020
Habari ID: 3473382
TEHRAN (IQNA) - Ufalme wa Saudi Arabia umesisitiza kwamba unaunga mkono uanzishwaji uhusiano kamili na kawaida na utawala wa Kizayuni wa Israel.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudia, Faisal bin Farhan Aal Saud ametoa kauli hiyo pambizoni mwa mkutano wa G20 mjini Riyadh na kuongeza kuwa, nchi yake daima imekuwa muungaji mkono wa uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni wa Israel kwa ajili ya kufikia amani ya kudumu.

Kabla ya hapo pia, Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia alikuwa ametangaza kwamba nchi yake inaunga mkono uhusiano wa kawaida na utawala ghasibu wa Kizayuni licha ya kwamba utawala huo pandikizi unafanya jinai kubwa dhidi ya Wapalestina.

Amma kuhusiana na matokeo ya uchaguzi wa Marekani, waziri huyo wa mambo ya nje wa Saudi Arabia amesema, ana yakini kwamba serikali ijayo ya Marekani itafuata siasa zile zile za huko nyuma za nchi hiyo kuhusu eneo hili na kwamba hakutokuwepo mabadiliko yoyote katika uhusiano wa Riyadh na Washington.

Matamshi hayo ya waziri wa mambo ya nje wa Saudia yametolewa katika hali ambayo, rais mteule wa Marekani, Joe Biden alidai kabla ya uchaguzi wa rais huko Marekani kwamba iwapo atashinda uchaguzi huo, ataangalia upya uhusiano wa Washington na Riyadh.

Tarehe 15 Septemba mwaka huu, Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Bahrain walitia saini makubaliano ya kutangaza uhusiano wa kawaida baina ya nchi zao na utawala ghasibu wa Israel.

Sherehe hizo zilizofanyika katika Ikulu ya Marekani, White House, zilihudhuriwa pia na rais wa Marekani, Donald Trump na Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala dhalimu wa Israel.

3473183

captcha