IQNA

Wanigeria waendeleza maandamano ya kutaka Sheikh Zakzaky aachiliwe huru

21:08 - November 25, 2020
Habari ID: 3473391
TEHRAN (IQNA) - Wananchi wa Nigera jana Jumanne waliendeleza maandamano yao katika mji mkuu wa nchi hiyo, Abuja, kushinikiza kuachiliwa huru kiongozi wa Harakati ya Kiislamu, Sheikh Ibrahim Zakzaky.

Katika maandamano hayo wananchi wa Nigeria wamelaani kuendelea kushikiliwa korokoroni Sheikh Zakzaky na mkewe.

Waandamanaji wamebeba mabango na picha za Sheikh Zakzaky ili kuonesha uungaji mkono wao kwa kiongozi huyo wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria.

Tarehe 13 Disemba 2015, jeshi la Nigeria liliivamia kituo cha tablighi cha Sheikh Zakzaky mjini Zaria, kikampiga risasi mwanaharakati huyo wa Kiislamu na kumtia mbaroni yeye na mkewe na tangu wakati huo linaendelea kumshikilia korokoroni, licha ya Mahakama Kuu ya Nigeria kutoa amri ya kumwachilia huru.

Jeshi la Nigeria liliwaua kwa umati mamia ya Waislamu wakati lilipovamia kituo hicho cha tablighi cha Sheikh Zakzaky. Miongoni mwa Waislamu waliouwa shahidi katika uvamizi huo wa jeshi la Nigeria ni watoto watatu wa kiume wa Sheikh Zakzaky.

Mwezi Agosti 2019, baada ya mashinikizo makubwa ya ndani na ya kimataifa, mahakama ya Nigeria ilitoa idhini kwa Sheikh Zakzaky na mkewe kwenda kutibiwa nchini India. Hata hivyo kutokana na usalama mdogo na kukosekana madaktari wa kuwaamini na pia kuhatarishwa usalama wa maisha yake, Sheikh Zakzaky na mkewe walikataa matibabu hayo na kuamua kurejea Nigeria.

Mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Abuja, maafisa usalama wa Nigeria walimkamata Sheikh Zakzaky na mkewe na kuwapeleka kusikojulikana.

Maandamano ya wananchi wa Nigeria yanaendelea ili kushinikiza kuachiliwa huru mwanaharakati huyo wa Kiislamu ambaye ni mtetezi wa wanyonge.

3937260

captcha