Kijana huyo aliuawa akishiriki katika maandamano ya amani ya kulaani jinai za utawala huo ghasibu.
Akizungumza kwa njia ya simu na baba ya kijana huyo, naibu kiongozi wa Hamas Saleh al-Arouri amelaani mauaji hayo ya kinyama ambayo yalitekelezwa na askari wa utawala haramu wa Israel.
Amesema Hamas na Wapalestina wote wataendelea na mapambano dhidi ya Wazayuni ambao wanakalia kwa mabavu ardhi za Palestina. Aidha amesema Wapalestina wataendeleza jitihada za kuuzuia utawala wa Kizayuni kuteka ardhi zaidi katika eneo la Ukingo wa Magharibi na pia watakabiliana na njama za kuuyahudisha mji wa Quds (Jerusalem).
Halikadhalika Arouri amesema mapambano na muqawama ndio njia pekee ya kukabiliana na uvamizi na jinai za Israel dhidi ya taifa la Palestina.
Kijana Mpalestina Ali Abu Alia, aliuawa Ijumaa kwa kupigwa risasi na askari wa Israel katika kijiji cha Al Mughair karibu na mji wa Ramallah ulio katika Ukingow wa Magharibi wa Mto Jordan.
Mjumbe wa Umoja wa Mataifa Mashariki ya Kati, (Asia Magharibi), Nickolay Mladenov, amesema amefadhaishwa na mauaji hayo. Ameongeza kuwa utawala wa Israel unapaswa kufanya uchunguzi huru na wa haraka kuhusu mauaji hayo ya kutisha na yasiyokubalika.