IQNA

Kiongozi wa Hamas: Kuanzisha uhusiano na Israel ni kuusaliti umma wa Kiislamu

22:13 - December 24, 2020
Habari ID: 3473488
TEHRAN (IQNA) - Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS amesema kitendo cha baadhi ya nchi za Kiarabu cha kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni wa Israel ni kuwasaliti wananchi wa Palestina na umma wa Kiislamu kwa ujumla.

Ismail Haniya amesema hayo katika ujumbe aliowaandikia zaidi ya viongozi 30 wa nchi za Kiislamu na Kiarabu na kusisitiza kuwa, kufanya wa kawaida uhusiano na utawala huo haramu ni kosa kubwa la kistratejia.

Amesema hatua hiyo ya baadhi ya nchi za Kiarabu ya kuanzisha uhusiano wa kawaida na Israel itakuwa na taathira hasi kwa maslahi ya umma wa Kiislamu na ni hatari kubwa kwa kadhia ya Palestina.

Haniya ameeleza bayana kuwa, suala la Palestina hivi sasa lipo katika hatari kubwa na linakabiliwa na changamoto tele kutokana na usaliti huo wa baadhi ya watawala wa Kiarabu wa kukubali kurubuniwa na kushinikizwa kuanzisha uhusiano na Tel Aviv.

Mapema mwezi huu wa Disemba, Morocco ilikuwa nchi ya nne ya Kiarabu kuanzisha uhusiano na utawala haramu Israel tokea mwezi Agosti wakati mtawala wa Marekani anayeondoka, Donald Trump alipoanzisha mkakati wa kuzishinikiza nchi za Kiarabu kuanzusha uhusiano na utawala huo bandia.

Mbali na Morocco, nchi zingine za Kiarabu ambazo zimeanzisha uhusiano na Israel hivi karibuni ni pamoja na Umoja wa Falme za Kiarabu, Bahrain na Sudan ambazo zimeanzisha uhusiano na utawala huo dhalimu katika fremu ya njama za Marekani-Kizayuni za kudhoofisha uungajo mkonowa nchi za Kiarabu kwa harakati za kupigania ukombozi wa Palestina. Nchi za Kiarabu ambazo zimekuwa na uhusiano na Israel kwa muda mrefu ni Jordan na Misri.

3943045

captcha