IQNA

Hamas yailaani Israel kwa kuzuia chanjo ya Corona kuwafikia Wapalestina Ghaza

20:21 - February 16, 2021
Habari ID: 3473654
TEHRAN (IQNA) Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas, imelaani kitendo cha utawala haramu wa Israel kuzuia dozi 2,000 za chanjo ya Corona kuwafikia wafanyakazi wa sekta ya afya katika Ukanda wa Ghaza.

Katika taarifa Hamas imesema hatua ya Israel kuendeleza mzingiro katika Ukanda wa Ghaza na kuzuia chanjo ya Corona kufika katika eneo hilo ni kinyume cha sheria za kimataifa.

Msemaji wa Hamas Hazem Qassem amesema hatua hiyo ya Israel ni jinai na ukiukwaji wa sheria za kimataifa pamoja na vigezo vya ubinadamu.

Mamlaka ya Ndani ya Palestina, yenye makao yake katika Ukingo wa Magharibi, ilikuwa imepanga kutuma chanjo ya Russia aina ya Sputnik V huko Ghaza.  Katika taarifa, Wizara ya Afya ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina imesema Israel imezuia chanjo hiyo kufikishwa Ghaza na imetoa wwito kwa Shirika la Afya Duniani (WHO) kulaani kitendo hicho cha Israel.

Msemaji wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina Ibrahim Melhem amesema WHO na taasisi zingine za kimataifa zinapaswa kuibebesha Israel dhima ya madhara yatokanayo na kuzuiwa chanjo kuingia Ukanda wa Ghaza.

Mamlaka ya Ndani ya Palestina imesema inataraji kupokea dozi milioni mbili za chanjo ya Corona kutoka wategenezaji mbali mbali kote duniani na pia kutoka kwa mpango wa Covax wa Umoja wa Mataifa.

/3474001

captcha