IQNA

Sri Lanka yafuta amri ya kuchoma moto miili ya Waislamu

20:41 - February 26, 2021
Habari ID: 3473685
TEHRAN (IQNA)- Kufuatia mashinikizo, serikali ya Sri Lanka imebatilisha uamuzi wake wa kuteketeza moto miili ya Waislamu waliopoteza maisha kutokana na Corona au COVID-19.

Sri Lanka imekuwa ikikosolewa kimataifa kwa amri yake ya kutetekteza miili ya watu wote ambao wanapoteza maisha kutokana na COVID-19 jambo ambalo ni kinyume cha mafundisho ya Kiislamu.

Uamuzi huo umechukuliwa baada ya Waziri Mkuu wa Pakistan Imran Khan kutembelea Sri Lanka ambapo inaaminika kuwa ameishauri serikali ya nchi hiyo kubatilisha amri ya kuteketeza moto miili ya Waislamu.

Hivi karibuni Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC) ilitoa wito kwa Sri Lanka kuheshimu haki za Waislamu kuzikwa kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu.

Yousef Al Othaimeen, Katibu Mkuu wa OIC aliyasema hayo wakati akizungumza katika Kikao cha 46 cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa. Amesema OIC inafuatilia hali ya Waislamu katika nchi zisizo za Kiislamu. Kwa msingi huo amesema OIC ina wasiwasi kuhusu Waislamu wa Sri Lanka kwani wananyimwa haki ya kuzikwa kwa mujibu wa mafundish ya Kiislamu wanapofariki kutokana na COVID-19. Amesema Shirika la Afya Duniani (WHO) limeshatoa maelekezo ya namna ya kuzingatia sheria za Kiislamu za maziko wakati wa kuwazika Waislamu waliopoteza maisha kutokana na COVID-19.

Mbali na Waislamu,  baadhi ya Wakristo nchini Sri Lanka pia wamekuwa wakilalamikia amri hiyo ya kuteketeza miili moto.

Inadokezwa kuwa tokea janga la corona lianze, maiti za Waislamu 200 waliofariki zimeteketezwa moto Sri Lanka kwa mujibu wa itikadi za Wabuddha na Wahindi ambao ndio wengi nchini humo.

/3956329

captcha