IQNA

Rais Rouhani: Iran na Pakistan zinasisitiza kuhusu kupambana na ugaidi, chuki dhidi ya Uislamu

19:37 - April 21, 2021
Habari ID: 3473838
TEHRAN (IQNA)- Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema Iran na Pakistan zinasisitiza kuhusu kushirikiana katika kupambana na ugaidi, chuki dhidi ya Uislamu na kudumisha usalama wa mpaka baina ya nchi mbili.

Rais Rouhani ameyasema hayo leo mjini Tehran alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Pakistan Shah Mehmodu Qureishi. Rais Rouhani pia amesisitiza udharura wa kudhaminiwa amani na uthabiti wa eneo kupitia mikakati ya kieneo, kudhaminiwa usalama wa mipaka ya Iran na Pakistan na kueleza kwamba, usalama ni wasiwasi wa pamoja wa nchi mbili hizi jirani, hivyo kuna haja ya kuimarishwa zaidi ushirikiano katika uwanja huo.

Ameashiria suala la umuhimu wa ushirikiano na Pakistan ikiwa nchi jirani ya Kiislamu na kusisitiza kwamba, kuna haya ya kustawishwa na kuimarishwa ushirikiano wa nchi mbili katika nyanja mbalimbali kama za kiuchumi na kibiashara na vilevile kupanuliwa ushiriikiano wa masoko ya mipakani.

Rais wa Iran ameashiria uamuzi wa Marekani wa kuondoa wanajeshi wake nchini Afghanistan na kwamba, uwepo wa vikosi hivyo haujasaidia chochote katika kuleta amani na uthabiti katika eneo la Asia Magharibi na kueleza kuwa, Iran na Pakistan zikiwa nchi muhimu jirani na Afghanistan na zenye taathira kuwa zinapaswa kushirikiana na kuwa na mchango muhimu katika mchakato wa amani wa Afghanistan.

Rais Rouhani ameashiria pia makubaliano ya hapo kabla baina ya nchi mbili, udharura wa kutekelezwa kivitendo makubaliano hayo na akatangaza utayari wa Iran wa kudhamini mahitaji ya Pakistan katika uga wa nishati.

Kwa upande wake Shah Mahmood Qureshi, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Pakistan ameutaja uhusiano wa Tehran na Islamabad kuwa ni wa kipekee, wenye thamani na wa kidugu na akasisitiza juu ya kupanuliwa zaidi ushirikiano huo katika nyanja zote.

3966302

Kishikizo: iran pakistan rouhani
captcha