Katika taarifa leo Alhamisi, Mohammad Javad Zarif Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amemuombolea Ahmed Jibril, mwanzilishi wa Harakati ya Wananchi ya Ukombozi wa Palestina (PFLP—GC).
Jibril ameaga dunia Jumatano akiwa na umri wa miaka 83 wakati akipata matibabu katika hospitali moja mjini Damascus, Syria. Alikuwa miongoni mwa walioammini kuwa mapambano ya silaha ndiuo njia pekee ya kukabiliana na utawala wa Kizayuni wa Israel na kukomboa Palestina.
Katika ujumbe wake Zarif amesema: "Nimesikitishwa na kifo cha mwanajihadi asiyechoka Bw. Ahmed Jibril Katibu Mkuu wa Kamandi Kuu ya Harakati ya Wananchi ya Ukombozi wa Palestina." Amesema kifo chake kimesikitisha yeye binafsi na marafiki wa mwendazake na wale wote wanaoipenda harakati ya muqawama.
Katika ujumbe wake, Zarif ameongeza kuwa, taifa madhulumu la Palestina limempoteza mwanajihadi na mwanamapambano ambaye alitumia umri wake kwa ajili ya kupigania ukombozi wa Quds Tukufu.
Kufuatia msiba huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ametuma salamu zake za rambi rambi kwa familia, viongozi na wanachama wa Harakati ya Wananchi ya Ukombozi wa Palestina. Aidha Zarif amemuomba Mwenyezi Mungu amrehemu mwendazake na aipe subira familia yake wakati huu wa majonzi.