IQNA

Hali nchini Tunisia baada ya waziri mkuu kuuzuliwa

19:42 - July 26, 2021
Habari ID: 3474129
TEHRAN (IQNA)- Vyombo vya habari vimearifu kuwa, jeshi la Tunisia limetuma vikosi vya jeshi katika mji mkuu wa nchi hiyo, Tunis kufuatia matukio ya karibuni na uamuzi wa Rais wa nchi hiyo, Kais Saeid wa kuwafuta kazi Waziri Mkuu na Spika wa Bunge.

Wanajeshi hao wametumwa katika mji mkuu wa Tunisia  ili kukabiliana na maandamano ya wananchi kufuatia uamuzi wa ghafla uliochukuliwa na Rais Kais Saeid wa nchi hiyo wa kumfuta kazi Waziri Mkuu Hichem Mechichi. Rais wa Tunisia aidha amefuta kinga ya kisiasa ya wabunge wote na kusitisha shughuli za Bunge. 

Wakati huo huo, vikosi vya usalama vya Tunisia vimewazuia waandamanaji kufika mbele ya makao ya Harakati ya An Nahdhah mjini Tunis na katika miji mingine ya nchi hiyo. Rached Ghannouchi Spika wa Bunge la Tunisia amekosoa uamuzi uliochukuliwa na Rais Kais Saeid akisema hatua iliyochukuliwa na rais ya kusitisha shughuli za Bunge na kumfuta kazi Waziri Mkuu Hichem Mechichi ni jaribio la mapinduzi dhidi ya mapinduzi, katiba na uhuru wa Tunisia. 

Televisheni ya al Jazeera yenye makao yao huko Doha, Qatar pia imeripoti kuwa, Muungano wa Wafanyakazi nchini Tunisia umewaalika viongozi wake wote katika kikao cha dharura ili kuchunguza uamuzi huo wa ghafla wa Rais Kais Saeid wa Tunisia. 

Wakati huo huo Rais wa Tunisia ameonya kuwa, atakabiliana na yoyote  atakayefanya chokochoko dhidi ya serikali.

Rais Kais Saeid jana usiku aliiitisha kikao cha dharura na makamanda wa jeshi na wa vyombo vya usalama na kuchukua uamuzi wa kumfuta kazi Hichem Mechichi Waziri Mkuu wa nchi hiyo na akachukua madaraka ya utendaji, kusitisha shughuli za Bunge na kuwafutia kinga ya kisiasa wabunge wote wa nchi hiyo. 

3475326

Kishikizo: tunisia mapinduzi
captcha