IQNA

Wanafunzi 115 waliohifadhi Qur’ani waenziwa Misri

13:02 - September 12, 2021
Habari ID: 3474285
TEHRAN (IQNA)- Sherehe imefanyika katika kijiji kimoja kaskazini mwa Misri kuwaenzi wanafunzi waliohifadhi Qur’ani Tukufu.

Kwa mujibu wa taarifa,  wanafunzi 115 waliohifadhi Qur’ani wameenziwa na kutunukiwa zawadi katika sherehe iliyofanyika katika kijiji cha Al Riyadh katika jimbo la Beni Suef.

Miongoni mwa walioenziwa ni wavulana na wasichana 80 na washiriki wengine 35 walio juu ya umri wa miaka 20 ambao wote wamehifadhi Qur’ani Tukufu kikamilifu.

Sherehe hiyo ilijumuisha matembezi ya wanakijiji waliosikika wakitoa nara za Allahu Akbar huku wakiwapongeza waliohifadhi Qur’ani.

Katika  utamaduni wa nchi nyingi za Kiarabu hufanyika matembezi maalumu yenye lengo la kuwapongeza na kuwaenzi waliohifadhi Qur’ani Tukufu kikamilifu.

Misri ni nchi mashuhuri kwa kuwa na idadi kubwa ya watu waliohifadhi Qur’ani na halikadlika pia ni mashuhuri zaidi kwa kuwa na wasomaji Qur’ani wenye vipaji vya kipekee.

Qur’ani Tukufu ni kitabu pekee kitakatifu ambacho kimehifadhiwa kikamilifu na waumini wake. Katika kila jamii ya Waislamu duniani kuna idadi kubwa ya watu waliohifadhi Qur’ani Tukufu kikamilifu.

Qur’ani Tukufu ina Juzuu au sehemu 30, Sura 114 na aya 6,236.

3996550

captcha