IQNA

Rais wa Iran ahutubu katika kumbukumbu ya kuuawa shahidi Qassem Soleimani

18:45 - January 03, 2022
Habari ID: 3474762
TEHRAN (IQNA)- Rais Ebrahim Raisi amesema, aliyekuwa rais wa Marekani Donald Trump ni muuaji na mhalifu mkuu wa mauaji ya kamanda Qassem Suleimani, kwa hivyo inapasa ashtakiwe na kuhukumiwa kuuawa kwa kisasi.

Akihutubia hadhara ya wananchi katika uwanja wa Sala ya Ijumaa mjini Tehran kwa mnasaba wa kumbukumbu ya mwaka wa pili tangu alipouawa shahidi Al Haj Qassem Soleimani, Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameihutubu Marekani na maadui wengine wa taifa la Iran: "nyinyi mlidhani tarehe 13 Dei (Januari 3) ndio siku ya mwisho ya Al Haj Qassem, lakini imethibiti hiyo ni dhana batili, kwa sababu tarehe 13 Dei imekuwa siku ya kuzaliwa upya Al Haj Qassem."

Seyyid Ebrahim Raisi ameongeza kuwa, Al Haj Qassem Soleimani alikuwa mgeni rasmi wa waziri mkuu wa Iraq lakini Wamarekani waliivunja heshima ya Iraq na wakaliua taifa zima.

Rais wa Iran amesema, "ikiwa utafanyika utaratibu wa kutayarisha mazingira ya kupandishwa kizimbani na kushtakiwa kiuadilifu Trump, Pompeo na wahalifu wengine katika mahakama ya haki; na jinai ya kutisha waliyofanya ikachunguzwa na wakapewa adhabu kwa matendo maovu waliyofanya, litakuwa jambo zuri sana; lakini lisipofanyika hilo, msiwe na shaka kuwa mkono wa kisasi wa umma utafanya kazi yake."

Rais Raisi amesema, kutokana na utambuzi aliokuwa nao na kwa kuelewa namna ya kuutumia uwezo na fursa, shahidi Qassem Soleimani aliibadilisha harakati ya Hizbullah ya Lebanon kuwa kambi ya muqawama kikanda na kimataifa na akaongezea kwa kusema: kutokana na Al Haj Qassem kuufahamu uwezo wa vijana, aliwaandaa na kuwaweka tayari kukabiliana na wimbi la Uistikbari kwa ari, ujasiri na ushujaa.

Seyyid Ebrahim Raisi amesisitiza kuwa shahidi Qassem Soleimani alikuwa Chuo cha Fikra na akabainisha kwamba: "chuo hiki cha fikra hakiwezi kufutwa kwa kombora; chuo cha fikra cha Al Haj Qassem kitabaki na kudumu.

Luteni Jenerali Qassem Soleimani, aliyekuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC), ambaye Januari 3 mwaka 2020 alielekea Iraq kwa mwaliko rasmi wa viongozi wa nchi hiyo, aliuliwa shahidi akiwa pamoja na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu Mkuu wa Kikosi cha Kujitolea cha Wananchi wa Iraq cha Hashd al Sha'abi na wanajihadi wengine wanane katika shambulio la kigaidi la jeshi vamizi la Marekani karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Baghdad. Hujuma hiyo ilitekelezwa kwa amri ya rais wa wakati huo wa Marekani, Donald Trump.

Kufuatia jinai hiyo, mnamo Januari 8 mwaka 2020, Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu lilichukua hatua ya kulipiza kisasi kwa kuvurumisha makombora kadhaa dhidi ya kituo cha kijeshi cha Marekani cha Ain al Assad nchin Iraq. 

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inasisitiza kuwa bado haijamaliza kulipiza kisasi mauaji ya Shahidi Soleimani na kwamba kuondoka askari wote wa Marekani katika eneo la Magharibi mwa Asia ndiko kutalipiza kisasi damu ya Luteni Jenerali Soleimani.

4025882/

Habari zinazohusiana
captcha