IQNA

Jamaica yatakiwa ilinde haki ya wanawake Waislamu wanaovaa Hijabu

15:47 - January 18, 2022
Habari ID: 3474822
TEHRAN (IQNA)- Mfanya biashara mwanamke Muislamu Mjamaica ametoa wito kwa serikali ya nchi hiyo kutekeleza sera ya kutowabagua wanawake Waislamu maeneo ya kazi na vituo vya elimu sambamba na kulinda haki zao.

Karema Muncey, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Home Choice Enterprises ameyasema hayo katika mahojiano na gazeti la Jamaica Observer ambapo amebainisha masikitiko yake kuwa, wanawake Waislamu Jamaica wamekuwa wakibaguliwa kwa kuvaa vazi kamili la Hijabu au mtandio kichwani wakiwa maeneo ya umma. Amesisitiza kuwa Hijabu ni vazi ambalo ni wajibu kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu.

Muncey pia amependekeza kuwa Jamaica iadhimishe Siku ya Kimataifa ya Hijabu ambayo imekuwa ikiadhimishwa duniani kote tokea Februari 1 2013.

Halikadhalika amesisitiza kuwa Waislamu ni kama raia wengine wa Jamaica na wana mchango wao mkubwa katika uchumi wa nchi hiyo. Amesisitiza kuwa wanawake Waislamu wana nafasi muhimu katika jamii na yeye kama Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Home Choice Enterprises ni mfano wa mchango wa wanawake katika jamii.

"Nimewaajiri watu 55 katika shirika langu na kwa njia isiyo ya moja kwa moja nimewaajiri watu wengine 100.  Tuna jaji Muislamu, Amina Maknoon ambaye aliteuliwa miaka kadhaa nyuma na huvaa Hijabu kamili."

Bi. Muncey anasema kuna karibu Waislamu 5,000 Jamaica wakiwemo wafanyakazi kutoka nchi kama vile na Nigeria na mataifa ya Kiarabu.

3477427

Kishikizo: waislamu jamaica hijabu
captcha