IQNA

Saudia yaua na kujeruhi watu 260 katika hujuma dhidi ya Yemen

19:38 - January 21, 2022
Habari ID: 3474833
TEHRAN (IQNA)- Vyombo vya habari vya Yemen vimetangaza kuwa ndege za kivita za muungano vamizi wa Saudi Arabia vimeshambulia nyumba za raia katika mji wa Magharibi wa Hudaydah na jengo moja la mahabusu kaskazini ya mji wa Sa'ada.

Kwa mujibu wa ripoti za awali, watu zaidi ya 200, wakiwemo watoto, wameuawa na kujeruhiwa katika mashambulio hilo lililotokea leo asubuhi.

Televisheni ya al-Masirah imeripoti kuwa ndege za kivita za Saudia zimeshambulia jela ya muda mjini Sa'ada na kuua na kujeruhi makumi ya watu, wakiwemo wahamiaji wa Kiafrika. Televisheni hiyo imeonyesha taswira za majeruhi katika hospitali ya al-Jamhuri mjini humo.

Ripota wa televisheni ya al-Mayadeen ya Lebanon nchini Yemen amesema, maiti 62 zimetolewa chini ya kifusi.

Gavana wa mkoa wa Sa'ada, Mohammed Jabir Awad amesema, hospitali zimejaa watu waliouawa shahidi na majeruhi na kwamba wana shida kubwa ya dawa na vifaa vya matibabu. Ameongeza kuwa, jumuiya nyingi za kimataifa zilishawahi kutembelea jengo hilo la mahabusu lililoshambuliwa na ndege za kivita za Saudia.

Awali televisheni ya al-Mayadeen iliripoti kuwa, raia wasiopungua sita wameuawa na wengine 18 wamejeruhiwa baada ya ndege za kivita za Saudi Arabia kushambulia maeneo ya nyumba za raia usiku wa kuamkia leo.

Kufuatia shambulio hilo la kinyama la ndege za kivita za Saudi Arabia, dhidi ya maeneo ya raia mjini Hudaydah, Muhammad Ali al-Houthi, mjumbe wa Baraza Kuu la Kisiasa la Yemen amesema, hujuma hiyo ni "jinai ya kivita" na "haisameheki." Inadokezwa kuwa watu karibu 60 wameuawa au kujeruhiwa katika hujuma hiyo ya Hudaydah wakiwemo watoto wadogo.

Katika ujumbe alioandika kwenye mtandao wa Twitter, Al-Houthi ameihutubu Saudia: "msingepaswa kuendeleza uchokozi na jinai hadi leo, kama mashambulio ya mabomu yangekuwa na tija. Inshalla mtashindwa Yemen, kama Marekani inayokupeni silaha na kukusaidieni, ilivyoshindwa Afghanistan".

4030137

captcha