IQNA

Uadui wa utawala wa Israel

Iran: Utawala wa Israel ni chanzo cha ugaidi na uharibifu Asia Magharibi

7:00 - June 20, 2022
Habari ID: 3475399
TEHRAN (IQNA)-Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema katika mazungumzo yake na waziri mwenzake wa mambo ya nje wa Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) au UAE) kwamba kuwepo utawala pandikizi wa Kizayuni katika eneo hili ndiyo sababu ya ukosefu wa utulivu na amani kama ambavyo ndio ulioleta vitendo vya kigaidi na uharibifu katika eneo hili zima.

Hossein Amir-Abdolahian amesema hayo Jumamosi wakati alipozungumza kwa simu na Sheikh Abdullah bin Zayed Al Nahyan, Waziri wa Mambo ya Nje wa Imarati kuhusu masuala ya pande mbili, ya kieneo na ya kimataifa.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amegusia pia kipaumbele kikubwa cha siasa za mambo ya nje za Jamhuri ya Kiislamu yaani majirani wa Iran na kuhimiza kuimarishwa uhusiano wa Tehran na Abu Dhabi katika nyuga zote, bila ya kuruhusu madola baki ya kigeni kuingilia masuala ya ndani ya eneo hili.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Umoja wa Falme za Kiarabu amesema katika mazungumzo hayo kwamba nchi yake na Iran zina manufaa mengi ya pamoja na ametilia mkazo wajibu wa kustawishwa na kuimarishwa zaidi uhusiano wa pande mbili.

Amesema, Imarati kamwe haitoruhusu upande wowote ule kufanya uharibifu ndani ya nchi yake na jirani zake kwani Abu Dhabi inaupa umuhimu mkubwa utulivu na usalama wa majirani zake.

Pande mbili za Iran na Muungano wa Falme za Kiarabu zimehimiza pia kuendelea mawasiliano ya pande mbili na kusaidiana katika kutatua masuala yao. 

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran aidha amemwalika waziri mwenzake wa Imarati kuitembelea Tehran kwa ajili ya kuimarisha zaidi uhusiano wa pande mbili.

3479359

captcha