IQNA

Ibada

Sala; Neno lenye umuhimu mkubwa katika Qur’ani Tukufu

23:59 - August 11, 2022
Habari ID: 3475610
TEHRAN (IQNA) – Sala ni moja ya nguzo za Uislamu na Waislamu wanaamini kuwa ibada hii ni daraja linalowaunganisha na Mwenyezi Mungu SWT. Kwa hivyo, Sala ni muhimu sana kwa kila Muislamu.

Kuna mapendekezo mengi kuhusu Sala katika Qur’ani Tukufu na pia kutoka kwa Mtume Muhammad (SAW) Neno "Salah" limetajwa mara 60 ndani ya Qur'an Tukufu huku yatokanayo na Sala yakitajwa mara 98; hii inaonyesha umuhimu wa kufanya ibada hii.

Katika Juzi ya kwanza ya Qur’an Sala imeashiriwa mara sita. Kwa mfano, aya zifuatazo kutoka katika Sura Baqarah zinataja fadhila za waumini na haja ya kutekeleza maombi na kuomba msaada wa Mwenyezi Mungu katika nyakati ngumu.

“Ambao huyaamini ya ghaibu na hushika Sala, na hutoa katika tuliyo wapa. (Aya  ya 3). " Na shikeni Sala, na toeni Zaka, na inameni pamoja na wanao inama." (Aya 43) “Na tafuteni msaada kwa kusubiri na kwa kusali; na kwa hakika jambo hilo ni gumu isipokuwa kwa wanyenyekevu." (Aya  ya 45)

Zaidi ya hayo, aya mbili zifuatazo kutoka kwenye Sura  hiyo hiyo zinawashauri Waislamu kuzingatia zaidi Sala katika kukabiliana na njama za maadui za kupinga Uislamu. “Na (Kumbukeni) tulipo funga agano na Wana wa Israili: Hamtamuabudu yeyote ila Mwenyezi Mungu; na muwafanyie wema wazazi na jamaa na mayatima na masikini, na semeni na watu kwa wema, na shikeni Sala, na toeni Zaka. Kisha mkageuka isipo kuwa wachache tu katika nyinyi; na nyinyi mnapuuza.” (Aya ya 83) “Na shikeni Sala na toeni Zaka; na kheri mtakazo jitangulizia nafsi zenu mtazikuta kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu anayaona mnayo yafanya.” (Aya ya  110)

Nukta muhimu katika aya hizi ni kwamba Salah inaambatana na matendo mengine ya faradhi ambayo kila Muumini anapaswa kuyafanya, ikiwa ni pamoja na Zaka, subira, kuwatendea memana kuwatunza wazazi n.k.

Kwa hiyo, Salah ni mlango wa njia ya kumtumikia Mwenyezi Mungu, na hukamilisha matendo mengine mema.

captcha