IQNA

Mbunge India atishia kubomoa misikiti New Delhi

12:28 - January 19, 2020
Habari ID: 3472386
TEHRAN (IQNA) – Mbunge katika chama tawala chenye misimamo mikali ya Kihindu cha Bharatiya Janata (BJP) nchini India ametishia kuwa, misikiti iliyojengwa katika 'ardhi ya serikali' katika mji wa New Delhi itabomolewa.

Parvesh Sahib Singh Verma, Mbunge wa Delhi Magharibi amesema iwapo chama cha BJP kitapata  ushindi katika bunge la kieneo basi misikiti yote ambayo amedai imejengwa katika ardhi ya serikali itabomolewa.

Uchaguzi wa Bunge la Delhi umepengwa kufanyika Februari 8 na matangazo ya uchaguzi huo wa viti 70 yanatarajiwa kutangazwa Februari 11.

"Ardhi ya serikali ambayo imetumika kujenga maeneo ya kidini itachukuliwa baada ya BJP kuunda serikali ya Delhi. Kuna malalamiko kuwa zaidi ya misiki 54 imejengwa katika ardhi ya serikali mjini Delhi. Orodha yatayari imeshakabidhiwa gavana," ameandika Verma kwa Kihindi katika ukurasa wake wa Twitter.

Hayo yanajiri wakato ambao katika wiki za hivi karibuni  maelfu ya watu wa India wamekuwa wakiandamana kupinga sheria ya uraia inayowabagua Waislamu.

Sheria hiyo mpya ya uraia inaruhusu kupatiwa uraia wahajiri wa jamii za Wahindu, Mabudha na hata Wakristo wanaotokea katika nchi jirani za Pakistan, Bangladesh na Afghanistan, huku ikizuia kupewa uraia Waislamu wanaotoka katika nchi hizo.

Hivi karibuni pia Watawala wa jimbo lenye idadi kubwa zaidi ya watu nchini India wamebadilisha jina la Kiislamu wa mji wa kihistoria ambao unajulikana kama Allahabad na kuupachika jina bandia la Kibaniani au Kihindu.

Mwaka uliopita pia  Mahakama Kuu ya India iliwapokonya Waislamu ardhi ya Msikiti wa kihistoria wa Babri na kuwakabidhi Mabiniani (Wahindi) eneo hilo ili wajenge hekalu lao.

Chama cha BJP kimekuwa kikichukua hatua kadhaa za kuwakandamiza Waislamu nchini India tokea kiingia madarakani mwaka 2014.

Jamii ya wananchi wa India inaundwa na kaumu na dini mbalimbali na watu wa nchi hiyo wamekuwa wakiishi kwa amani na maelewano. Uhuru na mafanikio ya nchi hiyo yametokana na ushirikiano na mshikamano wa kitaifa wa India. Kwa msingi huo zinazochukuliwa na Wahindu wenye misimamo ya kuchupa mipaka dhidi ya Waislamu kwa kisingizio chochote kile yanaweza kuitumbukiza hatarini amani na umoja wa India. Idadi ya Waislamu India inakadiriwa kuwa milioni 200 lakini Waislamu nchini humo wanakabiliwa na hatari kubwa kutokana na misimamo ya kufurutu ada ya chama cha BJP.

3470387

 

captcha