IQNA

Wamisri wamkumbuka qarii mashuhuri Mohamed Siddiq El-Minshawi

18:46 - January 21, 2020
Habari ID: 3472392
TEHRAN (IQNA)- Misri imeandaa hafla ya kumbukumbu ya kuzaliwa qarii mashuhuri wa Qur'ani Tukufu nchini humo Mohamed Siddiq El-Minshawi.

Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, Taasisi ya Darul Iftaa ya Misri imeandaa sherehe mnamo Januari 20 kwa munasaba wa mwaka wa 100 tokea alipozaliwa Qarii El-Minshawi ambaye alizaliwa mwaka 1920.

El-Minshawi alizaliwa katika mji wa Al Minshah katika jimbo la Sohag nchini Misri na alilelewa na kuinukia katika familia ya wasomaji Qur'ani. Alifanikiwa kuhifadhi Qur'ani Tukufu kikamilifu akiwa na umri wa miaka 8 na mwaka mmoja baadaya akaanza kujifunza kusoma Qur'ani kitaalamu.

Baada ya muda usio mrefu Minshawi alipata umashuhuri kama qarii ambaye alikuwa akitumia mbinu za Tarteel na Tahqiq katika usomaji wake.

Alisafiri katika nchi nyingi duniani kwa ajili ya usomaji Qur'ani zikiwemo  Indonesia, Jordan, Saudi Arabia, Syria, Iraq, Pakistan na Sudan.

Misri ni mashuhuri duniani kama nchi ambayo imeweza kutoa wasomaji bora zaidi wa Qur'ani Tukufu katika miongoi ya hivi karibuni.

Miongoni mwa wasomaji mashuhuri wa Qur'ani Misri ni pamoja na Abdul Basit Abdus Samad, Mohammed Siddiq Minshawi, Shahat Mohamed Anwar, na Mustafa Esmail.

3873275

captcha