IQNA

Hizbullah: Ujumbe wa Taifa la Iraq linalopinga Marekani umeifikia dunia

21:01 - January 25, 2020
Habari ID: 3472405
TEHRAN (IQNA) - Brigedi za Hizbullah ya Iraq zimesema kuwa mapinduzi ya wananchi wa nchi hiyo yataendelea hadi wavamizi wote wa Kimarekani watakapofurushwa kikamilifu nchini Iraq na katika eneo zima la Asia Magharibi.

Taarifa ya Brigedi za Hizbullah ya Iraq imesema Wairaqi wamethibitisha kuwa wana umoja na mshikamano katika suala la kupambana na ubeberu wa Marekani.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa, wananchi wa Iraq waliofanya maandamano ya mamilioni ya watu juzi Ijumaa wamewafikishia walimwengu ujumbe walioukusudia kwamba ubeberu wa Marekani hauna nafasi katika ardhi ya "Baynan Nahrain."
Siku ya Ijumaa mamilioni ya wananchi wa Iraq waliandamana katika mji mkuu wa nchi hiyo Baghdad wakitaka kuondoka nchini humo wanajeshi wa Marekani baada ya wanajeshi magaidi wa dola hilo la kibeberu kufanya shambulio la anga tarehe 3 Januari 2020 na kuua kikatili Luteni Jenerali Qassem Soleimani, Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC, Abu Mahdi al Muhandis, Naibu wa Mkuu wa Kikosi cha Kujitolea cha Wananchi wa Iraq, al Hashd al Shaabi na wenzao wanane. Wanajeshi wa Marekani walifanya ugaidi huo karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad.
Kwa kufanya maandamano makubwa siku ya Ijumaa, wananchi wa Iraq wamedhihirisha nguvu ya Uislamu na taifa kubwa la Iraq dhidi ya nchi vamizi Marekani na waitifaki wao.
Makundi ya muqawama wa Kiislamu, shakhsiya wa kidini na viongozi wa kisiasa na kitaifa wa Iraq wameyataja maandamano hayo dhidi ya uwepo wa wanajeshi wa Marekani nchini humo kuwa ni "Siku ya Mamlaka ya Taifa."
Tokea Marekani iivamie Iraq mwaka 2003, imekuwa ikitekeleza siasa za kuidhoofisha serikali ya nchi hiyo na kuizidishia matatizo, hasa ya kiuchumi na kijamii. Licha ya Wairaki kushiriki katika chaguzi kuu nne, lakini hawajakuwa na nafasi yoyote ya maana katika kuainisha mustakbali wa nchi yao na hili linatokana na uingiliaji wa moja kwa moja wa Marekani katika uendeshaji wa nchi hiyo. Kwa kuzingatia ukweli huo ni wazi kuwa maandamano ya leo Ijumaa ya Wairaki utakuwa ni mwanzo wa kuimarishwa msimamo na umoja wa kitaifa wa nchi hiyo kwa kuwa yatadhihirisha wazi azma na uamuzi wa makundi tofauti ya kisiasa ya Iraq kwa ajili ya kuhitimisha uvamizi wa Marekani katika ardhi ya nchi hiyo.

3874126

captcha