IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Walimwengu wamestaajabishwa na namna Iran inavyoyakabili mashinikizo makubwa na ya kinyama ya Marekani

18:59 - February 15, 2020
Habari ID: 3472474
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuhusu mahudhurio makubwa ya wananchi imara wa Iran katika maandamano ya Bahman 22, na katika kuusindikiza mwili wa shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani, aliyekuwa Mkuu wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, kwamba uthabiti mkubwa wa taifa la Iran wa kuyakabili mashinikizo makubwa na ya kinyama ya Marekani umewastaajabisha wafuatiliaji wa masuala ya kimataifa.

Ayatullah Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo leo mbele ya hadhara ya maelfu ya wasomaji kasida za kuwasifu Ahlul-Bayt (as) na mashairi ya maombolezo ya kuwakumbuka watukufu hao, aliokutana nao kwa mnasaba wa kuadhimisha kuzaliwa Bibi Fatimatu-Zahra (SA), binti kipenzi wa Bwana Mtume Muhammad SAW na mbora wa wanawake ulimwenguni.

Amesema moja ya majukumu muhimu iliyonayo jamii ya wasomaji kasida hao ni kueneza mtindo wa maisha wa Kiislamu na kuufanya ukite katika jamii na akasisitiza kwa kusema: Kama tunataka kulikabili wimbi la hujuma za kiutamaduni za adui kwa kuurejesha mtindo wa maisha kwenye mkondo sahihi na wa Kiislamu, njia pekee ni kuutamadunisha mtindo huo.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, moja ya mafundisho aali na matukufu ya dini na ya mtindo wa maisha wa Kiislamu ni utamaduni wa kutomuogopa adui na kutawakali kwa Mwenyezi Mungu; na akaongezea kwa kusema: Laiti katika siku za awali za Mapinduzi ingelisemwa kuwa Iran itakuja kufikia hatua ya sasa ya kiwango cha sayansi na teknolojia na nafasi ya kisiasa na ya ushawishi kieneo, hakuna mtu yeyote ambaye angeamini; lakini taifa la Iran lilimtegemea Mwenyezi Mungu na halikulihofu dola lolote, hivyo limeweza kufikia hatua hii ya maendeleo.

Ayatullah Khamenei ameashiria pia mipango inayoratibiwa na vituo vya kifikra pamoja na propaganda kubwa zinazofanywa na vyombo vya habari vya Magharibi ili kulishawishi taifa la Iran lilegeze msimamo na kuiridhia Marekani; na akasisitiza kwamba: Kwa rehma za Mwenyezi Mungu taifa la Iran hadi sasa limeweza kusimama imara, na baada ya hapa pia litasimama imara, lakini kusimama imara huko kunahitaji umiminaji wa kudumu wa nishati ya kimaanawi ndani ya jamii.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekumbusha kuwa, majukumu hayo yenye umuhimu mkubwa yanaihusu pia jamii ya wasomaji kasida za kuwasifu Ahlul-Bayt (as) na akabainisha kwamba: Kwa rehma za Mwenyezi Mungu, hali ya Jamhuri ya Kiislamu ni nzuri kwa kila upande, kwa sababu Mfumo wa Kiislamu una makamanda wazuri, vijana wataalamu wa elimu wenye moyo wa kazi, wanautamaduni wenye hima kubwa na ghera, wasanii pamoja na wananchi walio tayari kuchapa kazi katika nyuga zote; kwa hiyo kutokana na kuwa na vipawa na uwezo kama huo, kwa fadhila za Mwenyezi Mungu taifa la Iran litapata ushindi kamili na wa uhakika dhidi ya kambi kubwa ya adui.

3878796/

captcha